• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 PM
Mawakili wataka Uhuru na Ruto watangaze mali yao

Mawakili wataka Uhuru na Ruto watangaze mali yao

PETER MBURU na WAIKWA MAINA

MAWAKILI wanamtaka Rais Uhuru Kenyatta na naibu wake William Ruto pamoja na maafisa wakuu wa serikali watangaze utajiri wao wazi ili kudhihirisha wamejitolea kupambana na ufisadi kikamilifu.

Wanachama wa Chama cha Mawakili wa Kenya (LSK) tawi la Rift Valley wakiongozwa na mwenyekiti wao John Ochang’ walitaka pia Jaji Mkuu David Maraga, naibu wake, maspika wa bunge la taifa na seneti, mawaziri, magavana na watumishi wengine wakuu wa umma wafanyiwe uchunguzi wa hali yao ya kimaisha na pia watangaze utajiri wao kwa Wakenya.

Kulingana na mwanachama wa LSK, Bw Bernard Kipkoech Ng’etich, vita dhidi ya ufisadi vinafaa kuanza katika afisi kuu zaidi za serikali.

“Haifai iwe tu inalenga sehemu chache. Tunataka kuona juhudi za kupambana na ufisadi kuanzia katika afisi ya rais. Tunataka kuona rais akitangaza kwa hiari amepata kiasi kipi cha mali tangu alipoingia mamlakani,” akasema Bw Ng’etich.

Hata hivyo, Rais wa LSK, Bw Allen Gichuhi, jana alikiri ufisadi unahitaji suluhisho katika sehemu zote za uongozi lakini akasema LSK kitatoa msimamo wake rasmi baada ya baraza lake kukutana.

Mawakili wa Rift Valley walikuwa wakizungumza wakati wa uchaguzi wa wanachama wa tawi hilo katika Rift Valley Sports Club mnamo Jumamosi.

Kulingana nao, kama maafisa wa ngazi za juu serikalini hawatadhihirisha kujitolea kwao kupambana na ufisadi, hatua zinazoshuhudiwa sasa dhidi ya washukiwa wa ufisadi katika shirika la Huduma ya Vijana kwa Taifa (NYS) hazitazaa matunda.

Wabunge wawakilishi wa wanawake wa kaunti tatu pia waliunga mkono juhudi za kupambana na ufisadi.

Wakizungumza mjini Ol Kalou wikendi, Wambui Ngirici (Kirinyaga), Rahab Mukami (Nyeri) na Faith Gitau (Nyandarua) walitaka uchunguzi wa sakata ya NYS ufanywe kwa kina zaidi na kusiwe na ubaguzi.

“Kiwango cha fedha kinachotajwa mahakamani hakilingani na kile kilichoripotiwa kwa umma. Tunataka kuwe na uchunguzi wa kina na kila mmoja aliyehusika atajwe wazi. Tuantaka wahusika wakuu pia wafike mahakamani kushtakiwa na kuhukumiwa,” akasema Bi Ngirici.

You can share this post!

Yabainika gari la seneta lililodaiwa kuibwa lilitwaliwa na...

Niachie ugavana uingie mbio za Ikulu, Wavinya amwambia Mutua

adminleo