• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 9:50 AM
TUZO YA NOBEL: Sheria ambazo Raila anafaa kufuata kushinda tuzo

TUZO YA NOBEL: Sheria ambazo Raila anafaa kufuata kushinda tuzo

Na GEOFFREY ANENE

WAKENYA wamechangamkia hoja iliyowasilishwa na raia wa Uingereza Ali Abdi akitaka kiongozi wa upinzani Raila Amolo Odinga ateuliwe kuwa mshindi wa tuzo ya kifahari ya amani ya Nobel. Hata hivyo, licha ya kuwa wazo nzuri, inaonekana Mkenya huyu hakufuata taratibu.

Kwa mujibu wa tovuti ya www.nobelprize.org, jina la mpendekezaji pamoja na jina la mtu ama shirika linalopendekezwa kuwania tuzo hii yanafaa kuwa siri hadi miaka 50 ikamilike.

Shughuli ya uteuzi ya wawaniaji huanza mwezi Septemba. Huo ndio wakati Kamati ya Nobel ya nchi ya Norway inajiandaa kupokea maombi.

Maombi haya huwasilishwa na wabunge, serikali, na mahakama za kimataifa za sheria; machansela wa Vyuo Vikuu, maprofesa wa sayansi ya jamii, historia, falsafa, sheria na theolojia, viongozi mambalimbali wa taasisi za utafiti za amani na taasisi za masuala ya kigeni; washindi wa zamani wa tuzo ya Nobel; wanachama wa bodi ya mashirika ambayo yamepokea tuzo hii; wanachama wa zamani na wa sasa wa Kamati ya Nobel ya Norway; na washauri wa zamani wa wa taasisi ya Nobel ya Norway.

Februari ni mwezi wa mwisho wa kuwasilisha maombi hayo. Ili kutiwa katika orodha ya wawaniaji wa tuzo ya Nobel mwaka unaozungumziwa, kwa mfano mwaka 2018, uteuzi huwa unatumwa kwa Kamati ya Nobel nchini Norway jijini Oslo kabla ya Februari 1 mwaka huo.

Maombi yanayopokelewa baada ya Januari 31 saa sita usiku yanatiwa katika orodha ya kujadiliwa mwaka unaofuata. Katika miaka ya hivi karibuni, Kamati hii imepokea karibu maombi 200 kuwania vitengo tofauti vya tuzo ya Nobel.

Tovuti ya tuzo hii inasema kuna wagombeaji 330 mwaka 2018, watu 216 binafsi na mashirika 114. Idadi ya barua zinazopigia debe wawaniaji/mashirika wakati mwingine huwa juu kwa sababu mara nyingi zinakuwa zinaunga mkono wagombea ambao si tofauti.

Orodha fupi kisha huundwa kati ya Februari na Machi baada ya kamati kutathmini kazi ya mwaniaji. Kati ya Machi na Agosti, mshauri anapitia teuzi hizo.

Washindi wa tuzo ya Nobel huchaguliwa mwezi wa Oktoba. Kamati ya Nobel inafanya kazi hiyo kwa kupiga kura, mshindi akiwa mwaniaji aliyepata kura nyingi. Uamuzi huo wa kura na hauwezi kubadilishwa hata kwa kukata rufaa. Majina ya washindi wa tuzo hii ya amani ya Nobel kisha yanatangazwa.

Hafla ya kutuza washindi wa tuzo ya Nobel hufanywa Desemba 10 jijini Oslo. Washindi hupewa tuzo hiyo ambayo huandamana na medali ya Nobel na Diploma na cheti kinachothibitisha zawadi ya fedha iliyotolewa.

Kwa mfano, mshindi wa mwaka 2017 Shirika la kumaliza sila za nyuklia (International Campaign to Abolish Nuclear Weapons – ICAN) lilipokea Krona 9, 000, 000 (Sh102, 382,827 za Kenya). Marehemu Maathai alizawadiwa Krona 8, 218, 994 za Uswidi, ambazo zikibadilishwa kwa pesa za Kenya ni Sh93, 495,974.

Mshindi wa tuzo ya mwaka 2018 atatangazwa Oktoba 5 jijini Oslo nchini Norway. Atapokea zawadi Desemba. Tuzo hii imepeanwa kutoka mwaka 1901 isipokuwa miaka 1914-1916, 1918, 1923, 1924, 1928, 1932, 1939-1943, 1948, 1955-1956, 1966-1967 na 1972. Tangu tuzo hii ianzishwe mwaka 1901, washindi 131 wameipokea (watu 104 binafsi na mashirika 27).

Ni Mkenya mmoja pekee amewahi kushinda tuzo hii. Mwendazake Wangari Maathai aliibuka mshindi mwaka 2004. Mchango wake mkubwa katika maendeleo, demokrasia na amani yalimfanya kutawazwa mshindi.

Kutokana na taratibu iliyoelezewa na tovuti ya tuzo hii, inaonekana ombi la Abdi kutaka kiongozi Odinga ajumuishwe katika orodha ya wawaniaji wa mwaka 2018 liliwasili kuchelewa.

Abdi amemmiminia Bw Odinga sifa tele katika juhudi za kutafuta amani nchini Sudan Kusini pamoja na kutatua uhasama mkubwa uliokuwa ukitokota nchini Kenya baada ya Uchaguzi Mkuu mwaka 2017 kupitia mkataba wa amani na Rais Uhuru Kenyatta mnamo Machi 9, 2018, miongoni mwa masuala mengine mengi yakiwemo kupigania demokrasia barani Afrika.

Kufikia Julai 23 asubuhi, tovuti kadhaa nchini Kenya ziliripoti kwamba Wakenya 1, 870 walikuwa ametia sahihi ombi la Abdi kupigia debe Odinga kuwania tuzo hiyo.

You can share this post!

Magunia ya bangi yanaswa Nakuru

Kasisi motoni kwa kupora wanawake Sh1.3 milioni

adminleo