• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
Ashtakiwa kulangua wasichana wa kigeni

Ashtakiwa kulangua wasichana wa kigeni

Na Richard Munguti

MMILIKI wa kilabu kimoja maarufu jijini Nairobi alishtakiwa Jumatatu kwa ulanguzi wa wasichana tisa kutoka nchi za Nepal na Pakistan kufanya kazi za kuwafurahisha wateja wake kinyume cha sheria.

Mabw Shaikh Furoan Hussain na Abdul Waheed Khan walikanusha mashtaka manne dhidi yao ya ulanguzi wa binadamu na kukandamiza haki za wasichana hao kwa kuchukua pasipoti zao na kuzificha kinyume cha sheria.

Mabw Hussain , mwenye kilabu cha Balle Balle kilichoko mtaani Parklands walishtakiwa mbele ya hakimu mkuu katika mahakama ya Milimani Nairobi Bw Francis Andayi.

Walikanusha mashtaka ya ulanguzi wa bindadamu kisha wakili Cliff Ombeta akaomba waachiliwe kwa dhamana.

Wawili hao walishtakiwa kuwa kati ya Feburuari 19 na Julai 9 mwaka huu wakishirikiana na watu wengine ambao hawajafikishwa mahakamani waliwaingiza raia mmoja wa Pakistan na raia wanane wa Nepal humu nchini kwa njia ya udanganyifu.

Shtaka lilisema kuwa wasichana hao waliokamatwa wakicheza densi katika kilabu hicho kujipatia riziki.

Kiongozi wa mashtaka Bw Solomon Naulikha alimweleza hakimu kuwa wawili hao walitwaa pasipoti za wasichana hao tisa kwa lengo la kuficha idara ya uhamiaji uraia wa wasichana hao.

Washtakiwa hao walikabiliwa na shtaka jingine la kuwasaidia wasichana hao kuingia humu nchini kinyume cha sheria za idara ya uhamiaji.

Shtaka lingine la kuwaficha wasichana hao kinyume cha sheria katika mtaa wa Parklands Nairobi.

“Upande wa mashtaka unapinga washtakiwa hawa wakiachiliwa kwa dhamana ndipo kiini chao kuwaingiza wasichana hawa hapa nchini kijulikane,” akasema Bw Naulikha.

Alisema adhabu ya makossa waliyofanya washtakiwa ni kali na wakiachiliwa kwa dhamana washtakiwa watatoroka.

Aliomba mahakama iwazuilie washtakiwa gerezani hadi kesi inayowakabili isikizwe na kuamuliwa.

Bw Ombeta alisema dhamana ni haki ya kila mshtakiwa na kumsihi asiwaachilie washtakiwa kwa dhamana.

“ Washtakiwa ni raia wa Kenya. Mahala pao pa kuishi na kufanyakazi panajulikana,” alisema Bw Ombeta.

Alieleza mahakama mshtakiwa anaweza kunyimwa dhamana ikiwa ushahidi umewasilishwa kuthibitisha atavuruga utekelezaji wa haki.

“Naomba hii mahakama iwaachilie kwa dhamana kwa vile ni haki yao ya kikatiba,” alirai Bw Ombeta.

Bw Andayi aliamuru washtakiwa wazuiliwe gerezani akisubiri kutoa uamuzi wa ombi lao ya dhamana.

Katika mahakama hiyo hiyo, wakili alishtakiwa kuvunja vikombe na kuharibu sufuria na chakula na kusababishia mkahawa ulioko katika jengo la Jamia hasara ya Sh400,000.

Mohammed Salaani alishtakiwa pamoja na Bw Osman Godana Jillo na Abdulaziz Hassan Abdullahi.

Walikanusha shtaka dhidi yao baada ya Bw Andayi kukataa ombi la wakili Salaani la kusitisha akisomea shtaka.

Bw Salaani aliwakilishwa na Bw Muendo Uvyu ambaye alimsihi hakimu asitishe kesi dhidi ya Bw Salaani asuluhishe mambo kadhaa na afisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (DDP).

You can share this post!

Kalonzo aonya Uhuru kuhusu wandani wake

Polo ajuta kutomasa mama pima kazini

adminleo