• Nairobi
  • Last Updated April 18th, 2024 9:15 PM
Mtoto aliyenusurika mafuriko kimiujiza afadhiliwa masomo

Mtoto aliyenusurika mafuriko kimiujiza afadhiliwa masomo

Na CHARLES LWANGA

MWANAFUNZI wa Darasa la Tatu aliyepotea kwenye mto Tana baada ya boti la kuwaokoa waathiriwa wa mafuriko kuzama na kupatikana baada ya siku nane bila kuvamiwa na mamba na viboko sasa amebahatika kupata ufadhili wa kimasomo.

Naibu mkurugenzi wa Shirika la Msalaba Mwekundu (KRSC) Dkt Asha Mohamed na Bi Najat Ibrahim wa KRCS tawi la Malindi, walijitolea kumfadhili mtoto huyo, Khadija Mohamed hadi chuo Kikuu wakati wa sherehe za kuchangisha pesa kuwasaidia zaidi ya watu 86,000 waliyoathirika na mafuriko katika Kaunti za Kilifi na Tana River.

Kati ya watu watatu waliopotea kwa siku kadhaa baada ya boti hilo kuzama, Khadija ndiye pekee aliyepatikana hai baada ya kukwamilia gongo lililokuwa linaelea majini hadi alipopata usaidizi.

Babake, Bw Bakero Dube hangeweza kudhibiti machozi yake aliposimulia mamia ya wafadhili waliohudhila hafla kisa hicho cha Aprili 27 ambacho kilimwacha bintiye wa miaka 12 marehemu na mwingine kutoweka hadi leo.

Bw Dube aliyeambatana na mwanawe Khadija alisema Khadija ambaye ni mwanafunzi katika shule ya Galili huko Garsen alipatikana kilomita saba kutoka eneo walikozama.

“Niko hapa kusema asante kwa shirika hili la Msalaba Mwekundu kwa yale wamenitendea na nikupitia msaada wao tunaendelea kupata nafuu baada ya msiba huo,” alisema.

Wapiga mbizi wa Msalaba mwekundu walimpata Khadija akiwa mnyonge huku amekwamilia gongo kwenye kichaka kilichojaa maji kutokana na mafuriko.

“Boti letu lilizama baada ya kugongana na boti lingine lililokuwa linaokoa waathiriwa. Tayati nimemzika binti yangu mwingine wa miaka 12 aliyeokolewa na KRCS ambao walikuwa wamepoteza matumaini kabla ya kumpata Khadija, mwingine hajawahi kupatikana hadi wa leo,” alisema.

You can share this post!

Masharti makali yatolewa kulinda wanafunzi tamashani

Msigawanyike, Kalonzo ataachiwa urais na Uhuru Kenyatta...

adminleo