Dimba

Arsenal kuhitaji kupita mtihani wa PSG kwanza kabla ya kubeba taji lao la kwanza UCL

Na REUTERS May 7th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MABINGWA watetezi PSG waliagana sare ya 1-1 na Bayern Munich Jumatano na kufuzu kwa fainali ya Klabu Bingwa Ulaya (UEFA).

PSG walitinga fainali hiyo kwa jumla ya mabao 6-5 ikizingatiwa mechi ya mkondo wa kwanza walishinda 5-4 wiki iliyopita.

Ousmane Dembele aliiweka PSG mbele dakika tatu baada ya mechi kuanza huku Bayern ikionekana kuwa na ugumu kupenya safu ya nyuma ya mibabe hao wa Ufaransa.

Mvamizi Harry Kane aliwasawazishia kipindi cha pili muda wa ziada lakini bao hilo halikutosha hata kusababisha mchuano huo uingie muda wa ziada.

Sasa PSG itakutana na Arsenal kwenye fainali Mei 30, Budapest, Hungary baada ya The Gunners kupiga Atletico Madrid 1-0 mnamo Jumanne na kufuzu kwa jumla ya magoli 2-1.

Bayern ililenga kutinga fainali ya Uefa kwa mara ya kwanza tangu 2020 lakini sasa itabidi iridhike na Kombe la Ujerumani na Bundesliga msimu huu.

“Tulionyesha mchezo mzuri dhidi ya timu ngumu kama Bayern. Tumefurahi tumefika fainali ya pili ya Uefa na wapinzani wetu pia walikuwa wagumu ila mwishowe lazima kuwe na mshindi,” akasema Kocha wa PSG Luis Enrique.

Dembele ambaye alifunga mara mbili wiki iliyopita, aliujaza wavuni mpira wa Khvicha Kvaratskhelia ambaye pia alitoka na mabao mawili wiki jana.

Bayern ilianza kubisha na karibu ipate bao kupitia Michael Olise na Luis Diaz ila wawili hao walipoteza nafasi za wazi za kufunga.

Kipa Manuel Nuer ilibidi atoke kwenye lango lake na kupangua mpira wa kichwa uliokuwa umepigwa na Joao Neves dakika ya 33.

Mnyakaji mwenzake wa PSG Matvei Safanov pia alijipata pagumu alipolazimika kuokoa shuti ya chini ya Jamal Musiala kabla ya muda wa mapumziko.

Katika kipindi cha pili, PSG walisalia nyuma lakini walikuwa hatari katika uvamizi wa kushtukiza (counter attack).

Bayern walionekana kukosa ari na makali na hilo liliwezesha PSG kusalia nyuma japo walipata nafasi nyingine shtukizi kupitia Desire Doue na Kvaratskhelia dakika za jioni.

Mfungaji bora wa Bayern, Kane ambaye alikuwa amelemewa mchezoni alipata mwanya na kufunga bao dakika ya mwisho, hilo likiwa bao lake la saba kwenye mechi saba mfululizo za Uefa msimu huu.

Hata hivyo, bao hilo lake la 55 katika mashindano yote kwa Bayern, halikutosha na pia muda uliipa timu hiyo kisogo.

“Iwapo bao letu lingekuja mapema, mashabiki wangelipuka uwanjani na naamini matokeo yangekuwa vinginevyo,” akasema Beki wa Bayern Konrad Laimer.