Kombe la dunia kupeperushwa na Azam TV; huku KBC ya Kenya ikisalia bila kibali
HAKUNA kituo cha televisheni cha bila malipo nchini ambacho hadi sasa kimepata haki za kuonyesha mechi za Kombe la Dunia litakalochezwa kati ya Juni 11 na Julai 19 nchini Marekani, Canada na Mexico.
Kwa mujibu wa orodha ya kampuni za televisheni za kulipia za Azam TV, New World TV na SuperSport International ndizo pekee zitakazoonyesha muchuano hiyo nchini Kenya.
Kwa miaka mingi, Shirika la Utangazaji la Kenya (KBC) limekuwa likirusha baadhi ya mechi za Kombe la Dunia kupitia televisheni bila kulipia, jambo lililowezesha mamilioni ya Wakenya kufuatilia mashindano hayo bila kulipia.
Hata hivyo, KBC bado haijapata haki za kuonyesha mashindano ya mwaka huu kutokana na ukosefu wa fedha.
Afisa mkuu katika shirika hilo aliyezungumza kwa masharti ya kutotajwa jina alisema uamuzi kuhusu iwapo KBC itaonyesha mashindano hayo unatarajiwa kujulikana wiki hii.
Mnamo Machi 24, Kamati ya Bunge ya Mawasiliano, Habari na Ubunifu (COIC) ilionya kuwa Wakenya huenda wakashindwa kutazama mashindano hayo kupitia KBC kutokana na ukosefu wa Sh150 milioni zinazohitajika kununua haki za kuonyesha mechi hizo.
Kanuni za FIFA zinazitaka kampuni zinazoshikilia haki za utangazaji katika mataifa mbalimbali kuonyesha idadi fulani ya mechi watazamaji kulipia, ingawa kiwango hicho hutofautiana kutoka nchi moja hadi nyingine.
Katika Kombe la Dunia la 2022 nchini Qatar, KBC ilifanikiwa kupata haki za kipekee za kuonyesha mashindano hayo bili Wakenya kulipia.
Iwapo KBC haitapata haki hizo, mashabiki wa soka nchini watahitajika kutegemea vituo vya kulipia au majukwaa ya kidijitali yatakayotangazwa rasmi kabla ya kuanza kwa mashindano hayo.
Wakati huo huo, Fifa imefanya mabadiliko makubwa katika mkakati wake wa utangazaji kwa kuruhusu baadhi ya watengeneza maudhui ya Kombe la Dunia kuonyeshwa bila malipo kupitia YouTube kwa mara ya kwanza katika historia ya mashindano hayo.
Aidha, baadhi ya mechi kamili zitaruhusiwa kuonyeshwa kwenye chaneli rasmi za YouTube za televisheni zilizopata haki ya kuonyesha mechi hizo.