Kompany: Sasa ngojeni mvua ya mabao mkondo wa pili uga wetu wa Allianz Arena
BAYERN Munich wamesema wapo tayari kushuhudia tena mvua yao ya mabao watakapowakaribisha mabingwa watetezi Paris Saint-Germain katika mkondo wa pili wa nusu fainali ya Klabu Bingwa Ulaya (UEFA) wiki ijayo.
Hii ni baada ya timu hiyo kupoteza kwa mabao 5-4 kwenye mechi ya mkondo wa kwanza Ufaransa Jumanne usiku.
Mchuano huo ulishuhudia mabao tisa, mengi zaidi kuwahi kushuhudiwa kwenye nusu fainali ya Uefa tangu kipute hicho kianzishwe.
Bayern walitangulia kufunga lakini walilazimika kupambana vikali kupunguza pengo kutoka 5-2, wakifunga mabao mawili kipindi cha pili na sasa timu zote bado zina nafasi za kufuzu fainali zikikabiliana Jumatano ijayo
“Kutakuwa na mabao mengi mechi ya marudio. Mengi zaidi,” akasema Kocha wa Bayern Vincent Kompany huku akiwashaajisha mashabiki wa timu hiyo wajitokeze kwa wingi katika mkondo wa pili.
“Tuko nyumbani, tutakuwa na mashabiki 75,000 uwanjani. Hatutaki kelele tu, tunahitaji wapaze sauti yao juu kabisa kwa kuwa lazima tutinge fainali,” akaongeza.
Kocha huyo raia wa Ubelgiji yupo katika msimu wake wa pili na Bayern na tayari ameiongoza timu inayowania mataji matatu kuvunja rekodi kadhaa za mabao msimu huu.
Bayern, ambao tayari wametwaa ubingwa wa Bundesliga, wameweka rekodi mpya ya mabao 113 kwenye ligi hiyo huku wakiwa bado na mechi tatu za kuwajibikia.
Rekodi ya awali iliyodumu kwa zaidi ya nusu karne ilikuwa mabao 101 kutoka msimu wa 1971/1972.
Hii pia ni mara ya kwanza kwa wachezaji watatu wa Bayern, Harry Kane, Michael Olise na Luis Diaz kufikisha mabao 10 au zaidi pamoja na pasi za kufunga mabao katika msimu moja wa Uefa.
Kane, ambaye pia ni nahodha wa Uingereza aliyefunga Jumanne, tayari ana mabao 13 katika Uefa na pia anaongoza orodha ya wafungaji wa Bundesliga kwa mabao 33.
Bayern pia watakutana na VfB Stuttgart katika fainali ya Kombe la Ujerumani mnamo Mei 23.
“Ukiruhusu mabao matano katika Uefa, kwa kawaida unakuwa umetoka, lakini sisi tulifunga mabao manne Paris,” akajitetea Kompany.
“Tuna uwezo wa kufunga mabao, tumedhihirisha hilo na tutafanya hivyo tena nyumbani.”
PSG ilitoka nyuma na kushinda mechi hiyo kupitia mabao ya Khvicha Kvaratskhelia na Ousmane Dembele waliofunga mawili huku Joao Neves akiongeza goli jingine. Bayern walifungiwa na Kane, Michael Olise, Dayot Upamecano na Luis Diaz.
Kando na Bayern, Arsenal na Atletico walitarajiwa kuvaana baadaye jana kwenye nusu fainali nyingine ambayo mkondo wake wa pili utasakatwa Jumanne ijayo.