Habari za Kitaifa

Kuchangamkiwa ghafla kwa zoezi la usajili kutabadili ramani ya upigaji kura – Wachanganuzi

Na JUSTUS OCHIENG April 29th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

ONGEZEKO la ghafla la Wakenya waliojitokeza siku ya mwisho ya zoezi la usajili wa wapiga kura limefanya Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) ikaribie kufikia lengo lake la kusajili wapiga kura milioni 2.5 kuelekea uchaguzi wa 2027.

Zoezi hilo lililodumu kwa mwezi mzima lilichangamkiwa kote nchini, hasa na vijana.

Katika taarifa, IEBC ilikuwa imesajili wapiga kura wapya milioni 1.87, sawa na asilimia 75 ya lengo lake.

Mwenyekiti wa IEBC, Erastus Ethekon, alieleza matumaini kuwa pengo lililobaki lingezibwa kabla ya kufungwa kwa zoezi hilo, akisisitiza kuwa uhalali wa uchaguzi wowote hutegemea sajili kamili na sahihi ya wapiga kura.

Takwimu hizi zinajiri katika muktadha wa uchaguzi wa 2022, uliokuwa miongoni mwa chaguzi zilizowahi kuwa na ushindani mkubwa zaidi nchini.

Rais William Ruto alipata kura 7,176,141 dhidi ya kura 6,942,930 za mpinzani wake Raila Odinga, tofauti ikiwa ni kura 233,000 pekee.

Hivyo basi, hata mabadiliko madogo katika idadi ya wapiga kura wapya yanaweza kuwa na athari kubwa katika matokeo ya 2027.

Katika kipindi cha wiki moja tu kati ya Aprili 17 na 23, zaidi ya wapiga kura 505,344 waliongezwa kwenye sajili, hali inayoonyesha kasi kubwa ya kuchangamka kwa wananchi.

Aidha, wapiga kura 159,410 walihamisha vituo vyao vya kupigia kura huku wengine wakiboresha taarifa zao, ishara ya ushiriki mpana na hamasa ya kisiasa.

Kwa mujibu wa takwimu za kaunti, Nairobi inaongoza kwa kusajili wapiga kura wapya 209,965.

Inafuatwa na Kiambu, Nakuru na Kakamega, ambazo zinajitokeza kama maeneo muhimu ya kisiasa yenye ushindani mkali.

Kaunti nyingine zinazoonyesha ukuaji wa kasi ni Machakos, Bungoma, Meru na Kilifi. Kwa upande mwingine, Lamu na Isiolo zilisajili idadi ndogo zaidi ya wapiga kura wapya.

Mwelekeo huu unaonyesha kuwa ifikapo 2027, kaunti chache zenye idadi kubwa ya watu zitakuwa na ushawishi mkubwa katika matokeo ya uchaguzi.

Wachambuzi wanataja hali hii kama kuibuka kwa “kaunti kuu”, ambapo ushindi utategemea zaidi maeneo ya mijini na viunga vya miji badala ya ngome za jadi za kikabila.

Aidha, ongezeko la vijana waliofikisha umri wa kupiga kura tangu 2022 linaongeza hali ya kutotabirika.

Kundi hili halijafungwa sana na siasa za kikabila, bali linaangazia zaidi masuala kama gharama ya maisha, ajira na utawala bora.

Mchanganuzi wa siasa Profesa Gitile Naituli, anasema wapiga kura hawa wapya wanaweza kubadilisha kabisa mwelekeo wa uchaguzi ujao.

Naye mchambuzi wa siasa Dismas Mokua anasema kuwa ushiriki wa vijana pamoja na wazee unaonyesha kuwa uchaguzi wa 2027 utakuwa na uzito mkubwa kwa mustakabali wa nchi.

Kwa Rais Ruto, ongezeko hili ni upanga wenye makali kuwili, linatoa fursa ya kupanua uungwaji mkono lakini pia linaongeza ushindani, hasa kutoka kwa wapiga kura vijana. Kwa upinzani, ni nafasi ya kuvutia wapiga kura wapya.

IEBC inalenga kufikia wapiga kura 28.5 milioni ifikapo 2027.

Hata hivyo, wataalamu wanasisitiza kuwa si idadi pekee itaamua mshindi, bali mikakati ya kampeni, miungano ya kisiasa na uwezo wa kuvutia wapiga kura.