WALLAH: Akupaye pesa umchague ujue anakununua na anaweza kukuuza wakati wowote ule
WATAALAMU waliobobea katika falsafa za kisiasa wanasema, “Uongozi si nguvu wala uwezo wa kutumia vyeo na pesa za kutoa rushwa kuwanunua watu. Uongozi ni hekima, heshima na uadilifu wa kutumia sayansi ya akili za kujua kuishi na watu vizuri”.
Huo ndio uongozi bora.
Kiongozi mwema anayejitolea mhanga kuwasaidia watu kwa dhati na kuwatumikia kwa roho safi bila ubaguzi wala upendeleo ndiye kiongozi wa haki! Huyo haitwi kiongozi tu bali pia huitwa mkombozi.
Uongozi bora hauambatani na sifa mbovu kama vile ufedhuli, ubaguzi, ubadhirifu, kiburi wala ujeuri kwa watu anaowaongoza.
Kumbuka kuwaongoza watu si sawa na kuwatawala watu. Hata hivyo, siku hizi mtu yeyote anayeshinda katika uchaguzi huitwa kiongozi na kumbe ni mtawala.
Katika kutafuta uongozi na viongozi, kuna doa la matumizi ya pesa.
Kiongozi mkombozi mwenye nia njema ya kuwakomboa watu wake kunako mazingira magumu ya maisha si lazima atoe pesa kuwahonga watu ndipo wampigie kura.
Imani yake na upendo wake wa kujitolea kuwakomboa watu kwenye dhiki ndiyo malipo na zawadi kwa watu wake.
Mkombozi hahongi wala hahongwi.
Bila shaka hela zinazotolewa kuwagawia watu ili wamchague kiongozi huwa ni za kuwapumbaza akili na kuwafumba macho wasione uovu na ulaghai wa anayejitetea kuchaguliwa.
Husababisha macho na akili, vyote kuzama katika kutazama pesa tu. Ukae ukijua kwamba anayekupa pesa ili umchague, anakununua.
Na akitaka anaweza kukuuza!