Dimba

Tanzania yaandika historia kwa kuizamisha Afrika Kusini Wafcon

Na TOTO AREGE, AKIWA CASABLANCA July 29th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

Tanzania imeandika historia katika Kombe la Mataifa ya Afrika kwa Wanawake (WAFCON) 2026 baada ya kuichapa Afrika Kusini mabao 2-1 na kutwaa ushindi wake wa kwanza kabisa kwenye fainali za mashindano hayo.

Ushindi huo wa Kundi B uliopatikana Jumatatu katika Uwanja wa Moulay Rachid mjini Casablanca pia ni wa pili pekee kwa taifa la Afrika Mashariki katika historia ya WAFCON, na umefufua matumaini ya ukanda huo kutinga hatua ya robo-fainali kwa mara ya kwanza tangu Ethiopia ilipofanikisha hilo mwaka 2004.

Diana Msewa aliwapa Twiga Stars uongozi dakika ya 38 kabla ya Bambanani Mbane kusawazisha kwa Afrika Kusini katika muda wa majeruhi wa kipindi cha kwanza.

Mchezaji wa akiba Hasnath Ubamba aliibuka shujaa wa Tanzania kwa kufunga bao la ushindi dakika ya 86 na kuwapa Twiga Stars ushindi wa kihistoria dhidi ya mabingwa hao wa mwaka 2022.

Kocha Bakari Shime alisema ushindi huo umewapa wachezaji wake imani ya kushindana na timu bora barani Afrika.

“Kila timu hapa inapigania kufuzu Kombe la Dunia. Ushindi huu umetupa morali na kujiamini kuelekea mechi zilizosalia,” alisema Shime.

Kwa upande wake, kocha wa Afrika Kusini Desiree Ellis alikiri timu yake haikuwa katika kiwango kizuri licha ya kutengeneza nafasi nyingi.

Twiga Stars sasa Ina alama tatu sawa na Ivory Coast, iliyoichapa Burkina Faso mabao 4-1, lakini Ivory Coast inaongoza Kundi B kwa tofauti ya mabao mapema Jumatatu.

Tanzania ndilo taifa la pili pekee kutoka Afrika Mashariki kushinda mechi WAFCON baada ya Ethiopia kuifunga Afrika Kusini 2-1 2004, katika mechi ya hatua ya makundi.

Ushindi huo umeongeza matumaini ya ukanda huo kupata tena mwakilishi katika hatua ya mtoano baada ya zaidi ya miongo miwili.