Dondoo

Buda akabidhi polo bintiye na kikosi cha watoto bila kumuitisha mahari

Na KALUME KAZUNGU April 15th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

KATSEMERINI, Kilifi:

BUDA mmoja aliwaacha wanakijiji cha hapa na mshangao alipomkabidhi jombi mmoja bintiye na watoto watano bure bilashi.

Hii ni baada ya kuchoshwa na ugeni wa jombi huyo kila mara nyumbani kwake. Kila akiulizwa, jamaa alidai kuwa ni mchumba wa binti ya buda.

Cha kushangaza ni kwamba ugeni wa jombi ulianza miaka kadhaa iliyopita kabla ya binti kuanza kuzaa hadi sasa ambapo ni mama wa watoto hao watano.

Kila alipoulizwa, jombi alisema wakati wake wa kumuoa binti huyo rasmi haukuwa umejafika kwani bado anatafuta mahari.

Hivi majuzi lofa alipofika nyumbani kwa buda kama ilivyo ada yake alimpata mzee amesimama tisti nje ya nyumba.

Kando yake alikuwa binti na watoto wake watano.

“Sasa nimeshauriana na huyu binti yangu na wajukuu. Utaichukua hii familia yako mwende tu. Sina haja ya mahari. Kwa sasa wachukue roho safi ukawajibike,” buda alimwambia jombi huyo.