• Nairobi
  • Last Updated April 27th, 2024 4:26 PM
Ada za usafiri wa ndege kuongezeka kutokana na athari za Covid-19

Ada za usafiri wa ndege kuongezeka kutokana na athari za Covid-19

Na WINNIE ATIENO

WAWEKEZAJI katika sekta ya usafiri ya ndege wanakadiria ada za usafiri huo huenda zikawa ghali mno huku wakipambana kukabiliana na Covid-19.

Aidha Afisa Mkuu wa shirika la Kenya Airways Bw Allan Kilavuka ametangaza kuwa huenda ada ikawa ghali huku wakipambana kuhakikisha abiria hawakaribiani wanaposafiri kwenye ndege hizo.

Kulingana na Shirika la Afya Duniani (WHO), uvaaji wa barakoa, kuosha mikono kwa maji na sabuni na kujitenga na umma ni njia maluum ya kukabiliana na ugonjwa huo hatari unaosambaa kwa haraka.

Bw Kilavuka amesema mashirika ya ndege duniani yanaendelea kujadiliana namna ya kuhakikisha abiria hawakaribiani ili kuzuia maabukizi ya virusi vya corona.

Akiongea kwenye mkutano na wawekezaji mbalimbali duniani kujadili namna ya kuanza tena usafiri wa ndege na utalii, Bw Kilavuka amesema usafiri wa ndege utabadilika sana.

“Hali itakuwa tofauti sana; watu watavaa magwanda maalum, barakoa, na kila aina ya kifaa kujidhibiti dhidi ya maambukizi ya visuri vya corona. Tunakadiria asilimia 51 hadi 76 ya soko letu litapotea kuanzia sasa hadi mwishoni mwa Desemba. Lakini baadaye sekta itaimarika,” akasema Kilavuka.

Katika mkutano huo ambao uliwaalika zaidi ya watu 1,400 Bw Kilavuka alisema usafiri wa ndege siku za usoni utabadilika maradufu.

Bw Kilavuka ambaye ni mwanachama wa bodi ya magavana kwenye muungano wa uchukuzi wa ndege alisema walifanya mkutano Jumatatu wiki jana kwa kutumia vyombo vya kiteknolojia na mtandao kujadili maswala ya usafiri wa ndege.

Kwenye mkutano huo, alisema wawekezaji hao walijadili namna ya kuhakikisha sekta hiyo inaweka mikakati ya usafiri wa ndege kwenye sekta hiyo ulimwenguni ili kuzuia maambukizi.

You can share this post!

Walimu wa madrasa wahimiza wazazi watumie teknolojia...

Polisi wafyatuliana risasi na washukiwa wa al-Shabaab...

adminleo