Habari Mseto

COVID-19: Visa vipya ni 121

June 11th, 2020 Kusoma ni dakika: 1

Na SAMMY WAWERU

KWA muda wa kipindi cha saa 24 zilizopita, Kenya imethibitisha visa vipya 121 vya Covid- 19, idadi jumla ya wagonjwa ikigonga 3,215

Alhamisi, kwenye taarifa Wizara ya Afya imesema visa hivyo vimethibitishwa kutoka kwa sampuli 3,291 zilizokusanywa, zikakaguliwa na kufanyiwa vipimo.

“Kufikia sasa, tumepima jumla ya sampuli 106,247,” wizara hiyo imeeleza.

Imetuma taarifa kwa vyombo vya habari ikiwa ni pamoja na kuchapisha kwenye kurasa zake za mitandao ya kijamii.

Imechukua hatua hiyo kufuatia makadirio ya bajeti mwaka wa Fedha 2020/2021 yaliyokamilika kusomwa hivi punde na Waziri wa Fedha Ukur Yatani, kuchukua muda unaotumika katika kikao na wanahabari.

Nairobi imesajili visa 49, Busia (37), Mombasa (20), Kajiado (5), Migori (4), Kiambu na Kilifi (mbili kila moja), huku Murang’a na Nyeri zikiwa na kisa kimoja kila kaunti.

Wizara ya Afya pia imedokeza kwamba katika muda wa kipindi cha saa 24 zilizopita, wagonjwa 44 wameruhusiwa kuondoka hospitalini baada ya kuthibitishwa kupona, idadi jumla ya waliopona ikifika 1,092

Idadi jumla ya walioangamia nchini kwa sababu ya Covid-19 ni 92 baada ya wagonjwa watatu kufariki kipindi hicho cha saa 24 hivyo kumaanisha ipo haja ya Wakenya kuendelea kufuata masharti na kanuni za wizara.