• Nairobi
  • Last Updated April 27th, 2024 6:00 PM
Kagwe anapotosha Wakenya – Madaktari

Kagwe anapotosha Wakenya – Madaktari

WANDERI KAMAU na WAIKWA MAINA

MADAKTARI na matabibu wameilaumu serikali ya kitaifa na zile za kaunti kwa kutumia mbinu chafu kwenye juhudi za kutafuta utatuzi kwa mgomo wao unaoendelea.

Hapo jana, viongozi wa vyama vya wahudumu hao walisema serikali imekuwa ikitumia vitisho na uongo, licha ya maafisa wa Wizara za Afya na ile ya Leba kususia vikao wanavyoandaa kujadili kuhusu malalamishi yao.

Katibu Mkuu wa Chama cha Wahudumu wa Kliniki (KUCO), Bw George Gibore na mwenzake wa Chama cha Madaktari na Wahudumu wa Meno (KMPDU), Dkt Chibanzi Mwachoda, walimlaumu Waziri wa Afya Mutahi Kagwe, kwa “kuwadanganya” Wakenya kwamba serikali imetoa vifaa vya kuwasaidia kujikinga kuambukizwa magojwa (PPEs).

“Bw Kagwe anawadanganya Wakenya kuwa Mamlaka ya Kusambaza Dawa (Kemsa) imetoa PPEs kwa hospitali za umma lakini huo ni uongo. Wakati vifaa kama hivyo vinapotolewa, kuna fomu maalum ambazo hujazwa ili kuonyesha ni vingapi vilivyotolewa, na muda ambao vitatumika. Hakuna hospitali yoyote ya umma inayoweza kuonyesha fomu hizo kama ushahidi wa kupokea PPEs kutoka kwa Kemsa,” akasema Bw Gibore.

Wawili hao walisema Bw Kagwe anatumia uwongo ili kuwapaka tope na kuonyesha kuwa wao ndio hawataki kushiriki kwenye mazungumzo ya kutafuta mwafaka.

“Ni vibaya kwa waziri kutumia uongo kwenye mzozo kama huu ambao unawaathiri Wakenya,” akasema Dkt Mwachoda.Mnamo Jumanne, mwenyekiti wa Baraza la Magavana (CoG), Bw Wycliffe Oparanya aliziandikia barua serikali za kaunti akiziagiza kuwafuta kazi wahudumu wote ambao wanashiriki mgomo na kuwaajiri wengine.

Hata hivyo, wahudumu walisema jana hawatababaishwa hata kidogo na vitisho hivyo, kwani hata wale wataajiriwa watakumbana na matatizo wanayolalamikia.

Wakati huo huo, Kamati ya Bunge Kuhusu Afya, jana ilimtaka Bw Kagwe kusuluhisha utata uliopo kuhusu mgomo huo kwa kutoa vifaa vya PPEs kutoka maghala ya Kemsa.

Mwenyekiti wa kamati hiyo, Bi Sabina Chege, aliwalaumu magavana kuwa kikwazo kwenye utatuzi wa mgomo huo wakati Wakenya wanahitaji huduma za afya kwa dharura.

Bi Chege aliwatetea madaktari na matatibu, akisema baadhi ya matakwa yao yangeweza kutimizwa wakati walipotoa makataa ya kuanza mgomo huo.

You can share this post!

Uhuru awaruka Wakenya kuhusu ushuru nafuu

Njaa yatishia kusababisha vita Kaskazini mwa Kenya