• Nairobi
  • Last Updated April 27th, 2024 1:24 PM
Korti yaelezwa jinsi madaktari wa Cuba walivyotekwa nyara

Korti yaelezwa jinsi madaktari wa Cuba walivyotekwa nyara

Na MANASE OTSIALO

MAHAKAMA ya Mandera, Alhamisi ilisimuliwa matukio ya jinsi madaktari wawili wa Cuba mjini Mandera walivyotekwa nyara mnamo Aprili 2019.

Maelezo hayo yalijitokeza wakati wa kusikizwa kwa kesi ambapo dereva ameshtakiwa kuhusiana na utekaji nyara huo.

Jopo la mahakimu wa Nairobi wanaoendesha kesi hiyo Mandera, walizuru eneo la utekaji nyara huo ili kujifahamisha na mazingira ambamo tukio hilo lilitendeka.

Dkt Landy Rodriguez (mtaalam wa upasuaji) na Dkt Herera Correa (tabibu wa masuala ya jumla), walitekwa nyara katika uvamizi wa kutisha barabarani na watu wanaoshukiwa kuwa wanamgambo wa al-Shabaab, waliomuua afisa mmoja wa polisi aliyekuwa akiwasindikiza mnamo Aprili 12, 2019.

Hapo jana, Bw Ahmed Abdi, shahidi wa upande wa mashtaka alisimulia jinsi wawili hao walivutwa kutoka gari lao rasmi na kuingizwa katika gari aina ya Toyota Probox, lililoondoka kwa kasi kuelekea Somalia.

Bw Ahmed alikuwa akitoa ushahidi dhidi ya Bw Isaack Ibrein Robow, dereva anayeshukiwa kusaidia utekaji nyara wa madaktari hao wawili wa Cuba.

Bw Abdi, mfanyabiashara eneo hilo alisema alikuwa akisafirishwa kwa Tuktuk kisa hicho kilipotokea mnamo Ijumaa asubuhi.

“Nilikuwa ndani ya Tuktuk iliyokuwa ikiendeshwa na Barrow na bila shaka tulisikia milio ya risasi tulipokuwa tukisafiri kwenye barabara kuu mjini,” alisema.

Risasi

Mwendeshaji Tuktuk alitoroka na kumwacha Abdi anayeugua kisukari ndani ya kigari hicho chenye magurudumu matatu karibu na eneo ambapo risasi zilikuwa zikifyatuliwa.

“Niliona wanaume wawili wakitua upesi kutoka kwa gari lao lililokuwa mbele yangu. Walitoka upande wa kulia wa gari hilo kabla ya kutoweka,” alisimulia.

Bw Abdi alisema aligundua kwamba mmoja wa wanaume hao wawili alikuwa dereva wa gari la serikali lililokuwa limesimama mbele ya tuktuk lakini hakuweza kumtambua mwanamume wa pili.

“Dereva wa pick-up alikuwa amevalia kanzu nyeupe na ni mtu ninayemfahamu kwa sababu nimekuwa nikimwona akiendesha gari la serikali ya kaunti. Ni yeye alikuwa wa kwanza kutoka,” alisema.

You can share this post!

Spika wa Tanzania arai wabunge nchini Kenya watumie...

Kura: Seneta ataka majina bandia yawe halali debeni

adminleo