• Nairobi
  • Last Updated April 30th, 2024 8:55 PM
Mashine hizi zinatupotezea hamu ya uroda, wakulima wa chai walia

Mashine hizi zinatupotezea hamu ya uroda, wakulima wa chai walia

Na PETER MBURU

VIONGOZI wa wafanyakazi wa kuchuna majani chai wameunga mkono baadhi ya serikali za kaunti ambazo zimo mbioni kuunda sheria kupinga matumizi ya mashine za kuchuna majani chai, ama kuzitoza ushuru wa juu.

Wasema mashine hizo zimeleta hasara kuu ya kiuchumi na kiafya kwa wafanyakazi na kwamba, sasa wanaume wanaozitumia wameshindwa kutekeleza majukumu yao ya chumbani na kuwakolesha wapenzi wao tendo la ndoa.

Waliunga mkono serikali za kaunti Nandi na Kericho ambazo zinasemekana kuandaa miswada itakayohitaji mashine hizo kulipiwa ushuru na kuharamishwa kabisa.

Wakihutubia wanahabari mjini Nakuru jana, viongozi hao walisema kumeripotiwa visa vya wanaume wanaotumia mashine hizo kupoteza makali yao chumbani, mbali na kukumbwa na matatizo ya mgongo na kichwa.

“Wafanyakazi wanahitajika kubeba mashine kwa saa nyingi na hivyo wanaishia kuathirika na msukosuko wake kiafya.

Visa vya shida za mgongo, kichwa na hamu ya mapenzi kwa watumizi kwenda chini na hivyo kushindwa kutosheleza wapenzi wao vimeripotiwa,” akasema katibu mkuu mshirikishi wa wafanyakazi wa mashamba makubwa na kilimo nchini (KPAWU) Henry Omasire.

Kulingana na viongozi hao, kaunti ya Nandi inaandaa mswada utakaotoza ushuru mashine hizo, ilhali Gavana wa Kericho Paul Chepkwony naye yuko mbioni kulitaka bunge la kaunti yake kutunga sheria kuharamisha utumiaji wa mashine hizo.

Walisema hatua za kaunti hizo zitawaokoa wafanyakazi wengi masikini ambao wameathirika tangu mashine hizo ziagizwe nchini.

Walidai wafanyakazi 10,000 wamepoteza kazi tangu 2006, mbali na madhara ya kiafya.

Hii, waliongeza, ni kando na kuhatarisha usalama wa miji iliyoko karibu na mashamba ya majani chai.

 

You can share this post!

Ajuta kumbaka mpenziwe wa zamani

Mbinu ilizotumia Safaricom kuzoa faida ya Sh55 bilioni...

adminleo