• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 8:55 PM
Matokeo ya sensa kaunti yangu yanaogofya – Lonyangapuo

Matokeo ya sensa kaunti yangu yanaogofya – Lonyangapuo

Na Oscar Kakai

GAVANA wa Kaunti ya Pokot Magharibi, Profesa John Lonyangapuo amepuuzilia mbali matokea ya sensa ya kaunti hiyo akidai kinyume na matokeo, kaunti hiyo inaongoza kwa ongezeko la idadi ya watu.

Kulingana na ripoti ya sensa, kaunti hiyo ina watu 621,241. Gavana huyo ambaye alihudhuria sherehe ya kufuzu kwa walimu katika chuo cha walimu cha West Pokot alisema matokeo hayo ni ya kuogofya na atachukua hatua kali dhidi ya Idara ya Takwimu za Kitaifa Kenya (KNBS).

Alisema anaamini idadi ya watu wa kaunti hiyo ni kati ya 830,000 na milioni 1.2 kwa sababu ilikuwa ikiongoza kwa idadi ya watoto wanaozaliwa miaka iliyopita.

“Kwani nani waliua watu wetu? Nani anafanya kina mama wetu kutozaa?” aliuliza Prof Lonyangapuo.

“Inamaanisha wanawake wa Pokot Kaskazini ni tasa na wamekataa kuzaa kwa miaka kumi na wanaume wamekauka,” akaendelea kusema.

Viongozi wa maeneo mengi wamekuwa wakilalamika kuhusu matokeo hayo ya sensa na wengine wakitishia kushtaki KNBS ili ifafanue ilivyofikia takwimu hizo wakidai huenda kuna ulaghai ulifanywa.

Lakini KNBS imeshikilia kwamba ilifuata kanuni zote za kitaifa na kimataifa zinazosimamia sensa, na kwamba imejitolea kueleza kinaga ubaga ilivyofanya kazi yake kama itatakiwa kufanya hivyo.

Wanaopinga ripoti hiyo wanadai kuna njama ya kuwapunguzia mgao wa rasilimali, huku pia kukiwa na wasiwasi kwamba ripoti hiyo itatumiwa kuamua kama baadhi ya maeneobunge yanastahili kuendelea kuwepo au yaondolewe.

 

You can share this post!

Wambora ashtaki madiwani kwa kuzuia ukusanyaji ushuru

Makabiliano mapya baina ya madiwani yatarajiwa Nairobi

adminleo