• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 3:25 PM
Mwanamke alilia haki kufuatia mateso Uarabuni

Mwanamke alilia haki kufuatia mateso Uarabuni

Na MOHAMED AHMED

MACHOZI ya furaha yalibubujika kutoka machoni mwa mzee Ndolo Baya baada ya mtoto wake wa mwisho aliyekuwa anatumikia kifungo nchini Saudi Arabia kurudi nchini.

Mawazo ya Bw Baya, 71, kuwa ataenda kupokea maiti ya bintiye yaligeuka Jumapili baada ya kitinda mimba wake kurudi nchini salama.

Levina Mapenzi, 27, alirudi nyumbani baada ya kukaa nchini humo miaka minne.

Baada ya kufanya kazi kwa mwaka mmoja na nusu alikamatwa na kufungwa jela kwa madai ya kufanya zinaa.

Aidha katika mahojiano na Taifa Leo Jumapili,  Bi Mapenzi alidai kuwa alibakwa na dereva wa tajiri yake.

levina Mapenzi Ngolo akihadithia wanahabari Aprili 8, 2018 yaliyomsibu alipokuwa Saudi Arabia. Analilia haki baada ya kutupwa jela kwa mwaka mmoja nchini humo kwa kile alichokitaja kuwa madai ya uongo dhidi yake. Picha/ Laban Walloga

“Nilifungwa kwa madai ya kufanya ngono. Lakini sikuwa nimefanya hilo. Nilibakwa na jamaa huyo ambaye yeye alichapwa viboko kama ilivyo kulingana na sheria za kule,” akasema huku akitokwa na machozi ya uchungu.

Bi Mapenzi alitumikia mwaka mmoja jela ambapo alijifungua mtoto wake wa kiume aliyerudi naye baada ya kupatikana na masaibu katika nchi hiyo ambayo imeshutumiwa mara nyingi kufuatia kuteswa kwa Wakenya wanaoenda kufanya kazi hususan wanawake.

“Kwa sababu niliiambia mahakama kuwa nilifanyiwa dhuluma za kimapenzi ndio nikapewa adhabu hiyo ya kifungo cha mwaka. Nashukuru nimerudi salama lakini sikupata lile nililoendea,” akasema.

Bi Mapenzi aliondoka humu nchini mwaka 2014 bila ya ruhusa ya babake ili kutafuta riziki na aweze kukimu mahitaji ya mtoto wake wa kwanza aliyemuacha humu nchini.

Alieleza kuwa baada ya kupatikana na mimba ya miezi miwili na tajiri yake aliweza kuwapeleka yeye pamoja na mwanamume huyo polisi na baadaye kuhukumiwa.

 

You can share this post!

Gharama hii ya harusi na mahari inaogofya vijana kuasi...

Vijana wapanga kuvumisha utamaduni

adminleo