Ida aidhinisha Raila Jnr kugombea ubunge Kibra 2027
MJANE wa aliyekuwa Waziri Mkuu Raila Odinga, Ida Odinga, amemuidhinisha mwanawe Raila Junior kuwania kiti cha ubunge Kibra katika uchaguzi mkuu wa 2027.
Mama Ida alitoa kauli hiyo Jumatatu alipokuwa akiadhimisha miaka 76 ya kuzaliwa katika makazi yake Karen, Nairobi, sherehe iliyohudhuriwa na mamia ya wakazi wa Kibra.
Kwa mara ya kwanza, Mama Ida alizungumza wazi kuhusu nia ya mwanawe kuingia katika siasa, akisema ameamua “kumwachilia” kwa wakazi wa Kibra na viongozi wa Nairobi waliowahi kufanya kazi na Raila.
“Nyinyi watu wa Kibra mmeamua na sina la kufanya. Namwachilia mwanangu mikononi mwenu. Viongozi mlio hapa, mtunzeni, mumfundishe na mumwelekeze. Wengi wenu mlianza siasa na Baba. Mwonyesheni njia,” akasema Bi Ida.
Alisema Raila Junior anafaa kuendesha siasa safi bila matusi na vurugu, akisisitiza kuwa Kibra, ambayo ilijulikana kama “chumba cha kulala cha Baba”, ilikuwa nguzo muhimu katika safari ya kisiasa ya Raila.
Mama Ida pia aliwataka wakazi wa Kibra kudumisha amani na umoja licha ya tofauti zao za kisiasa.
Alisema hataweza kufanya kampeni kwa sababu ya wadhifa wake kama Balozi wa Kenya na Mwakilishi wa Kudumu katika Shirika la Mazingira la Umoja wa Mataifa (UNEP), lakini aliwataka wakazi kupendana na kushirikiana.
Raila Junior alisema aliamua kuwania Kibra baada ya kushauriana na wakazi na kwamba anafuata nyayo za babake ambaye alikuwa akishirikiana kwa karibu na wananchi wa kawaida.
Alisema siasa za babake zilijikita katika kushirikisha wananchi mashinani, kusaidia wanawake na watu wenye mahitaji.
“Nilikuwa uso wa Baba Kibra na nilimsaidia kutekeleza yale aliyoanzisha,” akasema Junior.
Ingawa alikiri kuwa Peter Orero ndiye mbunge wa sasa wa Kibra, Raila Junior alisema wakati umefika mahitaji ya wakazi yashughulikiwe na mtu anayefahamu eneo hilo vyema.
“Siasa za Baba hazitakufa. Lazima tuwepo, na nimesema nimeanza safari,” akasema.