• Nairobi
  • Last Updated May 4th, 2024 12:31 PM
Niliporwa mamilioni niliyochangiwa na Wakenya – Miguna Miguna

Niliporwa mamilioni niliyochangiwa na Wakenya – Miguna Miguna

Na CHRIS WAMALWA

MWANAHARAKATI wa vuguvugu la NRM, Miguna Miguna amedai kuibiwa Sh2 milioni alizochangiwa na Wakenya wanaoishi Amerika.

Dkt Miguna, ambaye anarejea nchini Jumatatu, alielekeza kidole cha lawama kwa kundi la Wakenya waliopanga mikutano kadhaa aliyoandaa katika mji wa Dallas katika jimbo la Texas kwa wizi huo uliofanyika Machi 10.

Bw Steve Aseno ndiye alikodi ukumbi wa mkutano na kupanga safari za Dkt Miguna.

Mwanasiasa huyo alitoa hotuba mjini Dallas, shughuli iliyofuatwa na mchango wa fedha za kuwalipa mawakili wake na kukarabati makazi yake katika mtaa wa Lavington, Nairobi yaliyoharibiwa na polisi waliotumwa kumkamata.

Dkt Miguna alidai kwa sauti ya juu kwamba, Bw Aseno ndiye alipora pesa zilizokusanywa katika mkutano wa Dallas.

Hata hivyo, Bw Aseno amekana madai hayo, akisema yeye ndiye alilazimika kutumia Sh100,000 zake mwenyewe.

Promota huyo alisema hafla ya kuchanga pesa ilifeli Dkt Miguna alipoanza kumshambulia kiongozi wa NASA Raila Odinga kwa kuamua kushirikiana na Rais Uhuru Kenyatta.

Bw Aseno alisema wafuasi wengi wa Bw Odinga ambao walikuwa wamethibitisha kuhudhuria shughuli hiyo walibadili nia Dkt Miguna alipoanza kushambulia Bw Odinga.

 

Adhabu ya kumkejeli Raila

“Ni wageni 114 pekee walihudhuria. Walitozwa Sh2,000 kila mmoja kama ada ya kungia ukumbini, Sh1,000 kwa kupiga picha na Miguna na Sh500 ili kupewa picha ya Raila. Kwa sababu Miguna alikuwa akitoa matusi dhidi ya Raila, hakuuza picha zozote wala kupata nafasi ya kupigwa picha na wageni waliohudhuria.

Hii ndio maana michango ilikuwa finyu zaidi,” Bw Aseno akesema kwenye mahojiano na “Taifa Jumapili”.

Promota huyo alisema alimkabidhi Dkt Miguna Sh119,500 zilizopatikana kutokana na mchango na Sh15,000 za mauzo ya picha, akisema haelewi ni kwa nini mwanasiasa huyo anadai kuwa yeye na wasaidizi wake walimwibia Sh2 milioni.

Wakati huo huo, Msomi Profesa David Monda anayeishi Amerika asema, huenda Dkt Miguna akakumbana na hali tofauti kabisa ya kisiasa baada ya Bw Odinga kukubali kushirikiana na Rais Kenyatta.

“Mandhari ya kisiasa nchini Kenyatta yamebadilika baada ya Rais Kenyatta kusalimiana kwa mkono na Bw Odinga. Miguna atabaini kuwa bila Raila hakuna NASA, na hata vuguvugu lake la NRM halipo tena.

Vijana wengi kutoka Luo Nyanza wanaweza kuhatararisha maisha yao kwa sababu ya Raila lakini hawawezi kufanya hivyo kwa Miguna,” akasema Profesa Monda.

Aliongeza: “Hulka yake ya makabiliano kila wakati, kando na ujasiri wake, ilidhihirika wakati wa ziara yake. Hali hiyo ilionekana wazi jinsi alivyopuuza maswali kutoka kwa washiriki na kuwashambulia wanasiasa akiwemo Bw Odinga. Amejitenga na wafuasi wa NASA,” alisema.

You can share this post!

Weta na Mudavadi waapa kusambaratisha ndoa ya Uhuru na Raila

Ziara ya Rais Uhuru na Raila mjini Kisumu yaahirishwa

adminleo