• Nairobi
  • Last Updated May 13th, 2024 9:17 PM
Polisi waliofutwa waamriwa warejeshe sare

Polisi waliofutwa waamriwa warejeshe sare

Na KNA

POLISI wa akiba nchini (NPR) waliopokonywa silaha na serikali, sasa wameamrishwa kusalimisha sare zote walizo nazo.

Kamishna wa eneo la Bonde la Ufa, Bw George Natembeya alisema polisi yeyote wa akiba nchini ambaye bunduki yake ilitwaliwa na ambaye huenda alikuwa amepewa sare ya serikali, ni sharti arudishe.

“Wanaozurura wakiwa wamevalia sare wanajifanya tu kama NPR. Serikali imefunga ukurasa wa kikosi cha zamani cha KPR ambapo walioteuliwa walikuwa wakiishi katika jamii wakiwa na bunduki,” alisema kamishna huyo.

Akizungumza mjini Eldoret Ijumaa wakati wa ziara ya kukagua miradi inayofadhiliwa na serikali kuu akiandamana na kamati ya maendeleo eneo hilo, Bw Natembeya alisema kikosi kipya cha NPR kitateuliwa na kupokea mafunzo na uteuzi wao hautafanywa kwa misingi ya eneo au kabila.

“Baada ya mafunzo polisi hao wa akiba wataishi kambini ambamo watasimamiwa na afisa mkuu wa polisi,” alisema.

Aidha, alitangaza kuwa watu wanaomiliki bunduki kinyume na sheria katika eneo la Kaskazini mwa Bonde la Ufa walikuwa na juma moja pekee kusalimisha silaha hizo kwa hiari kabla ya kupokonywa kwa nguvu.

“Kuanzia wiki ijayo tutapiga kambi Baragoi eneo la Samburu, Baringo, Turkana na Bonde la Kerio kuchukua silaha zote haramu zilizo mikononi mwa Wananchi. Ningependa kuhimiza mtu yeyote eneo hili anayemiliki bunduki kinyume na sheria kuisalimisha kwa hiari kwa serikali kabla ya muda wa makataa kuisha,” alisema.

You can share this post!

Wanasiasa lawamani kwa zogo la ngamia

Ziko wapi Sh30 bilioni makataa yakitimia Jumatatu?

adminleo