• Nairobi
  • Last Updated May 1st, 2024 11:29 AM
Pombe, mitambo ya kamari na bangi yateketezwa Thika

Pombe, mitambo ya kamari na bangi yateketezwa Thika

Na LAWRENCE ONGARO

WALANGUZI wa dawa za kulevya, watengenezaji pombe haramu na wachezaji kamari wamepewa ilani wajiondoe kwa biashara hizo ama wakabiliwe vilivyo na Serikali.

Kamishna wa eneo lote la Kati Bw Wilfred Magwanga amesema Alhamisi kwamba huu mwaka mpya wa 2020 ni wa kuangamiza maovu hayo yote bila kusita.

“Leo nimekuja na kikosi chote cha wakuu wa serikali hapa, na lengo letu kuu ni kuona ya kwamba maovu yote yanayotendeka eneo la Kati yanaangamizwa mara moja,” amesema Bw Magwanga.

Katika mkutano huo mitambo ya kuchezea kamari zaidi ya 200 ilichomwa pamoja na pombe haramu na dawa za kulevya.

Amesema tayari wamegundua sehemu zote zinazoendesha biashara hizo haramu na kwa hivyo, vitengo vyote vya usalama katika eneo hilo vitafanya juhudi kuona ya kwamba wahusika wote wanaoendesha kazi hiyo chafu wanatiwa nguvuni mara moja.

“Tutaweka doria katika mipaka zetu zote na kuhakikisha maafisa wa usalama wanakagua wale wote wanaoshukiwa kuwa ni walanguzi ama wauzaji wa dawa za kulevya,” amesema Bw Magwanga.

Wakati wa hafla hiyo iliyoendeshwa mjini Thika katika uwanja wa Community, Starehe, kamishna huyo alikuwa ameandamana na wakuu wote wa usalama kutoka hilo.

Himizo

Kamishna wa Kaunti ya Kiambu Bw Wilson Wanyanga amewahimiza wazazi kuwapeleka watoto wao shuleni bila kuchelewa.

“Hakuna sababu ya kutoa vijisababu kuwa huna uwezo wa kumpeleka shuleni mtoto wako. Ni vyema uwasiliane na watu wanaohusika ili uweze kupata usaidizi,” amesema Bw Wanyanga.

Amesema serikali iko tayari kupambana na walanguzi wa dawa za kulevya na wale wanaopika pombe vijijini.

Mitambo ya kamari. Picha/ Lawrence Ongaro

Afisa huyo hata aliwapa wananchi matumaini kwa kuwapa nambari maalum ya kupiga ambayo ni 988, iwapo watashuku jambo baya likitendeka katika maeneo wanakoishi.

“Kuna haja kubwa ya kuchunga mwenzako na ukiona jambo baya ama kusikia mara moja piga simu,” amesema Bw Wanyanga.

Mwenyekiti wa Nyumba Kumi ambaye anahusika na hali ya usalama katika mji wa Thika, Bw Charles Owila, amewashauri wananchi popote pale walipo kushirikiana na kamati yake ili kuripoti mambo maovu yanayoshuhudiwa katika makazi yao.

“Wengi wenu mnaelewa mambo mengi yanayotendeka katika makazi yenu lakini ubaya ni kuogopa kutoa habari kwa kamati yetu,” amesema Bw Owila.

You can share this post!

Mtoto alivyoibwa baada ya kuzaliwa, hospitali lawamani

Mzozo wa Iran na Amerika hautaathiri Kenya, ubalozi wa Iran...

adminleo