• Nairobi
  • Last Updated April 27th, 2024 6:47 PM
Siombi radhi, Wambua ni dume katili, Nzilani sasa asema

Siombi radhi, Wambua ni dume katili, Nzilani sasa asema

NA PIUS MAUNDU

Kwa mtu aliyejipata katikati ya zogo la kifamilia lililosambaa kote nchini, Jackline Nzilani anaonekana mwenye utulivu mwingi na mwenye roho ya kuwakaribisha watu.

Anaonekana mwenye upole na nafsi yake, hata ingawa ametuhumiwa kumsingizia aliyekuwa mume wake, Julius Wambua huku akimsababishia kufungwa gerezani nusura mwongo mzima.

Akiwa amevalia jaketi nyekundu, blauzi nyeupe na kufunga kitambaa chekundu kichwani, mama huyu mwenye watoto watano anatuongoza kule anakoishi Nairobi kwa ujasiri.

“Siogopi chochote na sijutii kile kilimfanyikia Wambua. Niko tayari kukabili korti na kutoa ushahidi na kuapa kuwa sikumshauri Mwende, mtoto wake adanganye,” asema Bi Nzilani mwenye umri wa miaka 46 anapoketi ili tumhoji.

Mara kwa mara anakatizwa na mwanawe mwenye umri wa miaka mitatu ambaye alimpata na mume aliye naye sasa. Mtoto huyu wa kijana anataka kuwekewa chai na hajui vile maisha ya kale ya mamake yalivyovutia vyombo vya habari.

Bi Nzilani ameshtakiwa kwa kumshauri mwanawe kudanganya kortini kuwa aliyekuwa mumewe alimdhulumu kimapenzi. Bi Nzilani anayejieleza kwa lugha ya Kiswahili iliyo na lafudhi ya lugha ya Kikamba, anasema yaliyo moyoni wake bila kujali huku akiwa haonyeshi hisia zozote za kujuta. Kwake maisha yanaendelea kama kawaida.

Alisimulia Taifa Leo Dijitali kuhusu kadhia za ndoa yake na mumewe Wambua na dhuluma ya kingono kwa bintiye ambayo anasimulia kwa urahisi mwingi kana kwamba yalifanyika jana.

Alisema hajutii hata kidogo kuhusu kufungwa kwa Wambua lakini anajutia hisia ya ‘kusalitiwa’ na watoto wake wawili wa kike; Mwikali na Mwende.

Bi Nzilani ambaye kwa sasa anafanya kazi kama kijakazi, anakumbuka alivyopigiwa simu na mwanawe wa pili, Musyoki ambaye alimweleza kuhusu alivyokiri Mwende.

Musyoki angemletea gazeti, ambalo bado analo, ya alichokiri Mwende huku akisema kuwa, alichokubali Mwende kilitokana na kumkataza kuacha shule ili aolewe.

“Tulikuwa tunaishi karibu. Mwikali na Mwende walikuwa wanaishi pamoja baada ya kumtaliki mume wake wa kwanza. Hapo ndipo mpango ukapangwa na nikagundua wakati ambapo nilianza kupata simu kutoka runinga ya Citizen,” anakumbuka.

Hata hivyo, Nzilani anasema kuwa hata ingawa Bw Wambua ameachiliwa, hataki kumuona tena kwani hakuna mapenzi kati yao.

“Siombi msamaha na hakuna radhi nitaomba kwani ushuhuda niliotoa bado ni wa kweli na alimbaka Mwende. Sikuwahi kumtembelea akiwa gerezani na siko tayari kurekebisha uhusiano baina yetu. Nishaendelea na maisha yangu,” akasema.

Kipande cha uchungu wake kinatokana na uhakika kuwa ndoa yao ilikuwa imegubikwa na mikasa mingi ambako alipigwa mara kwa mara na aliyekuwa mume wake wakati huyo.

Anakumbuka kuwa kile kilichoanza kama mapenzi matamu ya asali ya mwaka wa 1992 kiligeuka ghafla na kuwa shubiri huku vita vikichukua usukani kwa miaka 16 kabla ya kuivunja ndoa hiyo mwaka wa 2008.

Bi Nzilani anaonyesha kuwa Bw Wambua ni mwanamume mwenye matusi mengi, mwenye kutaka kudhibiti watu kwani angeangaza mienendo yake na alipokuwa na tashwishi alimgeukia na kumpiga.

Isitoshe, Nzilani haafikiani na uamuzi wa mahakama kuu ya kumuachilia Wambua kutoka gereza ya Kamiti kule ambako alipaswa kutumikia kifungo cha maisha.

“Korti haingemwachilia bila ya kushauriana nami. Niko tayari kurudi kwenye korti za sheria za Kithimani ili wasimame na ushuhuda wangu wa hapo awali. Sijifichi kutoka mtu yeyote,” akasema.

Kwake, ndoa yake haikuwa kitu angetamani kwa mtu yeyote kwani alikuwa anachapwa bila ya kutenda kosa lolote na hangeruhusiwa kutangamana na watu wowote kwa raha zake hata majirani.

Kwenda kanisa kulikuwa baada ya kuomba ruhusa. Anakanusha madai ya kuuza shamba la familia huku akisema kuwa ni bwana Wambua aliyeuza shamba hilo baada ya kumuoa mwanamke mwingine.

“Tulianza bila kitu hii ni baada yake kufukuzwa kutoka kwa nyumba ya mjomba wake. Tungelala kwa nyumba za majirani kwa kuwa hatukuwa na pahali pa kwenda. Ningevumilia kuchapwa lakini kile kilivunja ndoa yetu ni siku ambayo alinitishia mara kwa mara kuwa angeniua kwa panga. Hiyo ilikuwa mwisho. Niliondoka na sikuangalia nyuma.”

Baada ya kufika Nairobi,  Nzilani alijiunga na kanisa ya Wakorino baada ya kuwacha kwenda kanisa ya New Apostolic alipokuwa akishiriki akiwa mashambani.

Wakati Mwende alitoa ushuhuda wake, alimshtaki mamake kwa kumshauri kumsingizia babake. Bi. Nzilani hata hivyo anakanusha lawama hizo akisema hazina msingi.

“Sikumshauri Mwende kumsingizia babake. Tuliifuata ripoti ya daktari ambayo ilitoka katika hospitali moja ya kibinafsi jijini Nairobi,” akasema  Nzilani. Korti ilisikia kuwa Nzilani alibuni kesi hii ili kulipishia kile alipitia mikononi mwa bwana Wambua alipokuwa ameolewa naye.

Jaji George Odunga wa Mahakama ya Juu alisema kuwa alishawishiwa na ushahidi upya. Alihukumu kuwa kesi ya Wambua haikuhukumiwa vizuri na kuamuru kuwa kesi hiyo kusikizwa upya. Hata hivyo, Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (DPP) amesema kuwa hajaamua kama Wambua atahukumiwa upya kama alivyoagiza hakimu Odunga.

“DPP anapaswa kupitia kesi hiyo yote toka mwanzo na uamuzi uliotolewa kisha kuamua kama kesi hiyo itahukumiwa upya ama la kama alivyoagiza hakimu,” wakili wa DPP aliyejulikana kama Felista Njeru alieleza korti ya Kithimani, Jumatatu 21, 2020.

Jaji alimpa DPP mwezi kufanya uamuzi. Alikubali bwana Wambua kuachiliwa kwa dhamana iliyotolewa na mahakama kuu huku uamuzi wa DPP ukisubiriwa.

Kesi itatajwa Januari 25, 2021.

IMETAFSIRIWA NA WANGU KANURI

You can share this post!

Krismasi ya dhiki

Walemavu wafurahia zawadi ya Krismasi