• Nairobi
  • Last Updated May 5th, 2024 6:07 PM
Utatupwa ndani miezi 6 ukinaswa ukitema mate ovyo jijini Nairobi

Utatupwa ndani miezi 6 ukinaswa ukitema mate ovyo jijini Nairobi

COLLINS OMULO na JAMES MURIMI

MTU yeyote atakayepatikana akitema mate kwenye barabara ama kupenga kamasi bila kutumia kitambaa jijini Nairobi, atahukumiwa kifungo cha miezi sita gerezani au kutozwa faini ya Sh10,000.

Kwa mujibu wa mswada uliowasilishwa katika Bunge la Kaunti ya Nairobi, adhabu kama hiyo itapewa yeyote atakayebainika kushiriki ukahaba.

Mswada huo, ambao uko katika awamu ya kwanza, unalenga kuchukua mahali pa sheria za jiji la Nairobi, ambazo zilipitwa na wakati baada ya mfumo wa ugatuzi kuanza kutekelezwa.

Mswada huo umewasilishwa na diwani wa wadi ya Riruta, James Kiriba.

Wale ambao watapatikana wakiendesha magari au pikipiki kwenye vijia vilivyotengewa watumiaji miguu pia wataadhibiwa.

Kwenda haja kubwa ama ndogo kwenye barabara za jiji ama maeneo ya umma, kuwasha moto kwenye barabara za umma ama za jiji bila ruhusa ya Katibu wa Kaunti pia kutachukuliwa kuwa hatia.

Makosa mengine yaliyoorodheshwa na mswada huo ni kuacha mbwa ovyo kwenye barabara, kuosha ama kurekebisha gari kwenye barabara za jiji, kuvuta sigara kwenye maeneo ya umma na utingo kuwaita abiria kuabiri magari yao.

Kwa mujibu wa sheria hiyo, mtu ataruhusiwa kutengenezea gari lake barabarani tu ikiwa kuna hali ya dharura.

Kuchuuza, kuuza, kusambaza ama kutangaza maandishi yoyoye ama hafla katika barabara ya umma, kupiga kelele ama kutumia kengele, spika ama chombo chochote kile cha kupaaza sauti ama kuendesha gari ili kutangaza bidhaa bila kibali pia kumeorodheshwa kama kosa.

Hili pia litajumuisha kushiriki michezo kwa namna ambapo mtu anaweza kuharibu mali ama kusababisha majeraha.

Atakayefanya kosa lolote lililoorodheshwa hapo juu atakuwa kwenye hatari ya kuhukumiwa miezi sita gerezani, kupigwa faini ya Sh10,000 ama kupewa adhabu zote mbili.

Katika Kaunti ya Laikipia, yeyote atakayepatikana akienda haja ndogo, kutema mate ama kutupa taka katika maeneo ya umma atatozwa faini ya Sh5,000 ikiwa madiwani wataupitisha mswada huo.

Mswada unalenga kuhimiza umma kutilia maanani uhifadhi wa mazingira. Unaeleza kwamba yeyote anayepatikana akitupa vifaa vya ujenzi ovyo atatozwa faini ya Sh10,000.

“Atakayepatikana akitupa vifaa vya ujenzi kama mchanga, mawe ya kujengea ama kifaa kingine chochote cha ujenzi atapigwa faini ya Sh10,000,” unaeleza mswada ambao ushawasilishwa kwa Kamati ya Bunge kuhusu Fedha na Mipango.

Kwa mujibu wa kamati hiyo inayoongozwa na diwani Joseph Kiguru wa Wadi ya Igwamiti, mswada huo unalenga kuwaadhibu wale ambao hawatazingatia kanuni hizo.

“Mswada unalenga kuongeza mapato ya kaunti,” ikaeleza kamati.

Wale watakaopatikana wakipiga kelele ovyo kwa umma watatozwa faini ya Sh10,000.

“Hakuna yeyote atakayeruhusiwa kuwapigia wananchi kelele ovyo ikiwa hajapewa kibali maalum na idara husika kwenye kaunti,” unaeleza mswada.

“Yeyote atakayekiuka masharti hayo atatozwa faini ya Sh10,000,” unaeleza.

Mswada pia umeipa mamlaka Bodi ya Kukusanya Mapato ya Kaunti kuzikagua biashara zote kubaini ikiwa zimetimiza kanuni hizo.

Yeyote atakayeizuia kufanya ukaguzi kwenye biashara yake atatozwa faini ya Sh100,000.

You can share this post!

Walimu wataka kila shule ipewe mhudumu wa afya

LISHE: Biskuti za viazi vitamu