• Nairobi
  • Last Updated April 30th, 2024 1:01 PM
Utwaaji wa serikali ya Nairobi huenda usilete nafuu

Utwaaji wa serikali ya Nairobi huenda usilete nafuu

Na BENSON MATHEKA

HATUA ya serikali ya kitaifa ya kutwaa majukumu muhimu ya serikali ya kaunti ya Nairobi huenda isilete mabadiliko yoyote ikiwa yaliyoshuhudiwa miaka 37 chini ya utawala wa Kanu yatajirudia

Hatua hii imeibua kumbukumbu ya hali sawa mwaka wa 1983, wakati serikali ya Rais Daniel Moi kupitia aliyekuwa waziri wa serikali za wilaya Moses Mudavadi, ilipovunja baraza la jiji lililosimamiwa na aliyekuwa Meya Nathan Kahara.

Bw Mudavadi aliteua tume kusimamia jiji la Nairobi iliyojulikama kama Nairobi City Commission.

Ni chini ya tume hii ambapo unyakuzi wa ardhi ulichacha jijini hivi kwamba hata sehemu zilizotengewa vyoo vya umma zilitwaliwa na watu binafsi.

Tofauti na sasa ambapo Gavana Mike Sonko atabaki kuwa gavana, Bw Mudavadi aliwatimua Meya Kahara, Naibu wake Chadwick Adongo na madiwani wote pamoja na karani wa baraza la jiji George Wanjie. Wakuu wa idara tofauti pia hawakusazwa kwenye mabadiliko hayo.

Wadadisi wanasema bado ni mapema kusema kwamba hali sawa haitajirudia.

“Nafikiri mazingira sasa ni tofauti kwa sababu ya katiba ya serikali za kaunti. Hata hivyo kwa maoni yangu, madiwani wa kaunti ya Nairobi wanaelekea nyumbani kwa sababu sioni wakiwa na majukumu ya kutekeleza ikiwa watamtimua Gavana Sonko walivyopanga,” alisema mtaalamu wa masuala ya ugatuzi David Meto.

Wakati huo huo, serikali ilisema kwamba ilivunja baraza la jiji kwa sababu ya usimamizi mbaya uliosababisha ufisadi kukita mizizi. Huduma zilikuwa duni licha ya uchunguzi kubaini kwamba kulikuwa na zaidi ya wafanyakazi 17,000 baadhi hao wakiwa hewa.

Chini ya tume, matapeli waliteka shughuli za jiji na kukamua mapato yake huku huduma zikisambaratika zaidi jijini.

You can share this post!

China ilivyomfunga Uhuru mdomo

Jaji Smokin Wanjala augua homa ya nguruwe akiwa India

adminleo