• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 8:55 PM
Vuguvugu la Pwani latishia Raila

Vuguvugu la Pwani latishia Raila

Na MOHAMED AHMED

KINARA wa ODM Raila Odinga ana kila sababu ya kuwa na wasiwasi kufuatia kuanzishwa kwa vuguvugu la mageuzi eneo la Pwani baada ya baadhi ya viongozi kutishia kuunda chama kipya.

Vuguvugu hilo la mageuzi ambalo limekuwa na ming’ong’ono ya chini kwa chini kwa muda lilipata fursa ya kutoa kucha zake baada ya baadhi ya wabunge wa Pwani kueleza kutoridhishwa kwao na baadhi ya mambo yanayoendeshwa na chama cha ODM.

Mbunge wa Kilifi Kaskazini Owen Baya na mwenzake wa Malindi Aisha Jumwa sasa wameonekana kuwa viongozi wa gurudumu hilo la mageuzi ambalo linalenga uchaguzi wa 2022.

Wawili hao hivi majuzi waliongozana na wenzao jijini Nairobi kumkashifu Bw Odinga kwa kupigia upato mpango mpya wa ugavi wa mapato ambao utaumiza kaunti zote za Pwani kwa kuzipokonya fedha za maendeleo.

Wabunge hao wengine waliokuwa kwenye mkutano huo ni pamoja na Mohammed Ali (Nyali), Michael Kingi (Magarini), Sharif Ali (Lamu East), Andrew Mwadime (Mwatate), Khatib Mwashetani (Lunga Lunga), Jones Mlolwa (Voi) Paul Katana (Kaloleni) na Benjamin Tayari (Kinango).

Kwa jumla, kaunti hizo za Pwani zinatazamiwa kupoteza takriban Sh1 bilioni iwapo mswada huo utapitishwa. Hata hivyo wiki hii Bw Odinga alionekana kubadilisha msimamo huo na kupinga mswada huo wa fedha.

Hata hivyo, mpango wa kuanzishwa kwa vuguvugu hilo Jamvi la Siasa limegundua kuwa limeletwa na msururu wa matukio ambayo viongozi, wasomi na wakazi kwa jumla kuona kuwa kwa muda sasa kanda ya Pwani limekuwa likipitia shida kuntu mikononi mwa chama cha ODM ambacho kimekiunga mkono kwa muda.

Kabla ya mzozo wa masuala ya fedha, Bw Baya alikuwa ameeka wazi lalama kuhusiana na ODM kutowapa nafasi za kamati wabunge wa Pwani ambazo zilipatikana hivi majuzi baada ya wabunge wa Jubilee kuondolewa.

Lalama hizo zilifuatwa zile za baadhi ya wabunge kusemekana kufungwa mdomo na uongozi wa vyama na kutoweza kuunga mkono mswada wa mbunge wa Nyali Mohammed Ali wa kumuondoa waziri wa uchukuzi James Macharia.

Kufuatia hayo, wabunge hao wameeleza haja ya kuwepo kwa chama cha Pwani ambacho kitakuwa kinaipa sauti eneo la Pwani na kuhusika kwake katika siasa za 2022.

Sasa, wabunge hao wameanza kutoa mwito kwa baadhi ya magavana wa Pwani na kuwataka wawaunge mkono kwenye msukumo huo.Wiki hii, Bi Jumw alitoa mwito kwa Gavana wa Kilifi Amason Kingi na kumtaka ajiunge naoi li kuwekeza kwenye chama cha Pwani.

“Gavana Kingi toa shaka, toa hofu na uungane nasi. Safari ya kuunganisha Wapwani imeng’oa nanga. Sisi viongozi wa Pwani na wakazi tumejipanga na hakuna kurudi nyuma,” Bi Jumwa alisema katika mkutano wa hivi majuzi uliofanyika eneo bunge lake la Malindi.

Siku moja baadaye, Bw Baya naye akamtembelea Gavana wa Kwale Salim Mvurya ambapo waliongea kuhusiana na suala hilo la ugavi wa pes ana vugu vugu hilo la mageuzi.

Baada ya mkutano huo katika afisi za Bw Mvurya ambaye ni mwenyekiti wa Jumuiya ya Kaunti za Pwani (JKP), gavana huyo alisema kuwa iwapo Pwani itaungana basi kutakuwa na urahisi wa kuendesha ajenda zao katika siku za usoni.

“Tulikubaliana kuwa ni lazima tuungane sote ili tuhusishe kila mmoja katika safari hii ya mageuzi ya Pwani,” akasema Bw Baya.

Kulingana na mchanganuzi wa siasa za Pwani Profesa Hassan Mwakimako viongozi hao wa Pwani wamepata fursa ya kuongea yale ambayo wameogopa kusema kwa muda sasa kwa sababu ya vizuizi vinavyowekwa na uongozi wa chama tofauti ambavyo wapo ndani yake.

Alisema kuwa ni bayana kuwa viongozi hao pamoja na wakazi wamejiona kutengwa na kutosikika kwa sababu ya kukosekana kwa umoja wao kupitia chama.

“Ni wazi kuwa hata magavana walikuwa na nia hiyo hapo awali lakini wakanyamaza. Wabunge hao wameonekana kupata nafasi ya kueleza mawazo ya wengi ya wakazi wa Pwani,” akasema Profesa Mwakimako.

Aliongeza kuwa iwapo viongozi hao watashikana kweli basi watakuwa na nafasi ya kubwa zaidi ya kusikika kisiasa katika mwaka wa 2022.Hata hivyo, azma hiyo ya baadhi ya viongozi hao bado haijaleta pamoja viongozi wote kwani kuna wale ambao wanalemea upande wa Bw Odinga.

Miongoni mw ani mbunge wa Mvita Abdulswamad Nassir ambaye ni rafiki wa karibu wa Gavana Hassan Joho na ambao mara nyingi huwa na usemi sawia kwenye masuala ya siasa.

Akizungumza katika hafla ya uzinduzi wa mradi wa maendeleo eneo la Tudor wiki hii, Bw Nassir aliwashutumu viongozi ambao wametishia kutoka chama cha Bw Odinga na kuwataja wao kutokuwa wanachama thabiti wa chama hicho cha ODM. “Viongozi hawa hawajawahi kuwa waaminifu wa chama cha ODM.

Baadhi yao hata hawapo kwenye orodha ya wanachama wa ODM, hivyo basi sielewi ni kwa nini wanaendelea kutaja ODM,” akasema Bw Nassir.

Kwengineko, mwenyekiti wa Ngumu Tupu Hassan Chitembe ambalo ni vugu vugu linalomuunga mkono Bw Odinga alisema kuwa viongozi hao wanaotishia chama cha ODM hawana nguvu zozote za kisiasa za kumtishia kiongozi huyo.

Bw Chitembe ambaye ni mwanasiasa mkongwe wa Pwani alisema kuwa viongozi hao wameinuliwa kisiasa na Bw Odinga hivyo basi ni lazima wampee heshima yake.

“Pwani haitaki vyama vipya. Hao wanasiasa wanaopiga kelele kutaka vyama vipya ni kwa sababu wamekosa mwelekeo. Sisi watu wa Kwale tutasimama na Bw Odinga maana tunamtambua yeye kama kiongozi wetu,” akasema Bw Chitembe.

You can share this post!

Vigogo wa Nasa wapigana makumbo wakijipendekeza kwa Uhuru

Mombasa hakuna raha tena – utafiti

adminleo