• Nairobi
  • Last Updated April 30th, 2024 1:01 PM
Wafanyakazi wa kaunti wakosa ujira wa Februari

Wafanyakazi wa kaunti wakosa ujira wa Februari

Waziri wa Fedha Henry Rotich. Picha/ Maktaba

Na SILAS APOLLO na KENNEDY KIMANTHI

MAELFU ya wafanyakazi wa kaunti hawajapokea mishahara yao ya Februari huku serikali hizo za ugatuzi zikikabiliwa na upungufu mkubwa wa pesa, na kuathiri utoaji huduma na utekelezaji miradi.

Kaunti nne zimewaandikia wafanyakazi wao barua za kuwafahamisha kuhusu kucheleweshwa kwa mishahara yao ya Februari, kwa sababu hazijapokea pesa kutoka kwa Serikali ya Kitaifa.

Kaunti hizo za Kericho, Taita Taveta, Kilifi na Busia, katika barua hizo, zimekiri kuwa na mifuko mikavu na kuomba muda zaidi. Zilisema mishahara ya wafanyakazi hao italipwa tu baada ya Serikali ya Kitaifa kutoa pesa, hali ambayo imeshuhudiwa katika nyingi ya kaunti zingine 43 zilizosalia.

Haya yanajiri huku Waziri wa Fedha Henry Rotich – ambaye wiki jana alidokeza kwamba serikali imeishiwa na pesa, isipokuwa Sh200 bilioni za mkopo wa Eurobond ulioidhinishwa mwezi jana – akishauri wizara na idara za serikali kuweka mikakati mikali ya kudhibiti ubadhirifu wa fedha.

Hapo nyuma, magavana walitumia ovadrafti za benki kulipa mishahara ya wafanyakazi lakini mbinu hiyo ilishutumiwa na Wizara ya Fedha ambayo ilishauri wakuu hao wa kaunti kupata idhini yake kabla kufuata mkondo huo wa kuchukua mikopo.

“Hii ni kufahamisha kwamba mishahara ya Februari 2017 itacheleweshwa kwa sababu Wizara ya Fedha imechelewa kutoa pesa,” alisema Katibu wa Kaunti ya Kericho Joel Bett katika barua kwa wafanyakazi.

Huko Kilifi, Katibu wa Kaunti Benjamin Chilumo aliwaomba wafanyakazi kuwa watulivu akisema gatuzi hiyo inatazamia kuwalipa mishahara katika kipindi cha wiki moja ijayo.

Alieleza Bw Chilumo: “Hii ni kuwafahamisha kuwa mishahara ya Februari 2018 itachelewa. Hii imetokana na kucheleweshwa kwa fedha za Desemba za mgawo wa kaunti kutoka kwa Wizara ya Fedha, pesa ambazo tulikuwa tumepanga kuzitumia kulipa mishahara ya Februari.”

Haya yanajiri huku magavana wakionya kuwa kaunti zinatatizika kutekeleza majukumu yao kwa sababu ya kucheleweshwa kwa fedha hizo, miezi mitatu kabla kukamilika kwa mwaka wa sasa wa fedha.

Mwenyekiti wa Baraza la Magavana Josphat Nanok alisema Wizara ya Fedha ilikuwa imetoa asilimia 33 pekee ya fedha hizo kinyume na asilimia 75 zilizotarajiwa kufikia sasa, na kwamba mpango wowote wa kukosa kutoa pesa zote Sh18 bilioni kwa kaunti kutasababisha huduma kusitishwa.

“Kaunti zinakumbwa na mzozo mbaya wa kifedha miezi mitatu tu kabla kukamilika kwa Mwaka wa Fedha 2017/18. Pesa kidogo tulizopokea kufikia sasa zimelipa mishahara na gharama zingine za matumizi ya kawaida,” akasema Bw Nanok.

Ni kaunti za Nairobi, Narok na Trans-Nzoia pekee zimepokea zaidi ya nusu ya mgao wao wa Sh8.7 bilioni, Sh3.2 bilioni na Sh2.8 bilioni mtawalia.

Kaunti 24 zimepokea asilimia 45 ya mgawo huku zingine 20 zikipokea chini ya asilimia 25.

Kaunti iliyopokea kiwango kidogo sana kufikia sasa ni Elgeyo-Marakwet (Sh833,520,000 milioni).

You can share this post!

Joho awapongeza Raila na Uhuru

Walimu sasa waacha kutumia vitabu vipya

adminleo