Waiguru: Sikuomba Gachagua msamaha, matamshi yangu yalifasiriwa vibaya
GAVANA wa Kirinyaga Anne Waiguru amepuuza madai kuwa alimwomba aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua msamaha akisema matamshi yake yalifasiriwa vibaya na kuingizwa siasa na upinzani.
Akiongea wakati wa mchango wa kuwainua akina mama Kaunti ya Kwale, Bi Waiguru alisema kuwa alionyesha tu masikitiko iwapo baadhi ya Wakenya walikuwa wamekasirishwa na mienendo ya serikali.
Hasa gavana huyo alisisitiza kuwa hakuelekeza msamaha kwa mtu yeyote binafsi.
“Sikumwomba mtu yeyote msamaha. Nilisema tu kama kuna watu ambao wanahisi wamekosewa na serikali, basi tunasikitikia hilo. Matamshi hayo hayafai kufasiriwa hivyo na kuingizwa siasa,” akasema Bi Waiguru huku akisisitiza kuwa ataendesha kampeni kali ili Rais William Ruto achaguliwe tena.
Aidha alisisitiza kuwa yeye ni mwaaminifu kwa UDA na kupuuza uvumi kwamba alikuwa akipanga kuhamia chama kingine na kuondoka serikalini.
“Nitasalia UDA na kuunga mkono serikali kwa sababu tunamakinika kumuunga mkono Rais Ruto kutokana na maendeleo anayowafanyia Wakenya,” akaongeza.
Kiongozi huyo alisema rais amesambaza miradi ya maendeleo kwa usawa kote nchini na raia wanastahili kuwa wavumilivu naye anapoendeleza miradi zaidi.
“Rais ana mpango kwa taifa hili na tayari tunaweza kuona miradi ya maendeleo ikifika kila pembe ya nchi. Hatua huchukua muda na wananchi wanastahili kumpa muda wa kutekeleza ajenda yake,” akasema.
Aliwataka Wakenya wahakikishe kuwa UDA inawahi ushindi katika duru ya kwanza ya kura mwakani.
“Huu ni mwanzo tu wa ngoma kwa sababu tutazunguka kote nchini kufanya kampeni kali kuhakikisha kuwa rais anashinda katika awamu ya kwanza. Upinzani hauna ajenda zozote za kuendeleza nchi,” akasema Bi Waiguru.
Kwenye hafla hiyo aliandamana na Gavana wa Kwale Fatuma Achani, mwenzake wa Mombasa Abdulswamad Nassir, Waziri wa Madini Hassan Joho na viongozi wengine kutoka ukanda wa Pwani.
Bi Waiguru pia alimfanyia Bi Achani kampeni akimsifu kutokana na rekodi yake ya maendeleo kwa miaka mitatu amekuwa uongozi wa kaunti.
Bi Achani naye alimrejelea Bi Waiguru kama kiongozi ambaye baada ya kumaliza muhula wake wa pili, anastahili kuukwea ngazi hadi katika siasa za kitaifa.
Kwa miaka mingi, eneo la Pwani limekuwa ngome ya marehemu Raila Odinga kisiasa ambako katika kila uchaguzi tangu 2007 amekuwa akipata zaidi ya asilimia 60.
Viongozi wa ODM na UDA ambao walihudhuria hafla hiyo waliapa kuwa watazima upinzani kuingilia ngome zao na kuwahi viti vya kisiasa.
Bw Nassir alisema kuwa umaarufu wao upo juu kwa sababu viongozi wa UDA na ODM wamekubali kuungana kurindima ngoma ya Rais Ruto.
Mbunge wa Likoni Mishi Mboko alisema baada ya uteuzi wa Bw Joho kwenye baraza la mawaziri, rais amepata uungwaji mkono wa viongozi wa ODM na wafuasi wa chama hicho.
Kiongozi wa Wengi kwenye Seneti Aaron Cheruiyot alieleza kuwa rais anamakinikia kusambaza miradi ya maendeleo kote nchini kwa usawa.