• Nairobi
  • Last Updated April 30th, 2024 10:55 AM
Walimu sasa waacha kutumia vitabu vipya

Walimu sasa waacha kutumia vitabu vipya

Na JOSEPH WANGUI

WALIMU wamewacha kutumia vitabu vilivyosambazwa na serikali kwa mtaala mpya wakisema kuwa maelezo yake ni hafifu.

Katibu wa Chama cha Walimu wa Sekondari (Kuppet), kaunti ya Laikipia, Bw Ndung’u Wangenye alisema walimu wamewacha kutumia vitabu vilivyopendekezwa na serikali kwa sababu ya kuwa na makosa na kukosa maelezo ya kutosha ya kuwafunza wanafunzi.

“Walimu wanazuia kutumia vitabu kwa kuwa maelezo yake ni hafifu na wanafunzi wana uwezekano wa kutofanya vyema katika mitihani ya kitaifa ikiwa watatumia vitabu hivyo,” alisema Bw Wangenye, ambaye pia ni mratibu wa Kundi la Walimu wa eneo la Mt Kenya.

Alifichua kuwa walimu wanawashauri wazazi kununua vitabu vingine vya kusoma vyenye maelezo zaidi ili kuongezea kwa vile vilivyotolewa na serikali.

Bw Wangenye pia aliwasihi wachapishaji 100 ambao walichaguliwa na serikali kuchapisha na kusambaza vitabu hivyo, kuajiri watu wenye utaalam wanapounda maelezo na kurekebisha makosa kabla ya kusambaza nakala nyingine mpya.

Katibu huyo alieleza kuwa hakuna umuhimu wa kuendesha mfumo kwa sababu ya unalenga ujuzi badala ya ufahamu.

Alisema kuwa utekelezaji wa mtaala mpya na usambazaji wa vitabu umeharakishwa na kwamba wizara ya Elimu ilikosa kushauriana na wadau wengine katika sekta.

“Wazazi wanaamini kuwa elimu inastahili kuwa ya bure na kila kitu kutolewa na serikali. Wanalalamika baada ya kuambiwa wanunue vitabu vya Kiingereza na Kiswahili kwa fasihi na vitabu vingine kama ‘logarithm’, ramani na kikokotoo maalum,” aliongeza.

Pia alieleza kuwa wazazi walidhania kuwa serikali itatoa vitabu vyote.

“Serikali ilitoa taarufa ya kisiasa kwamba itatoa vitabu vyote. Lakini ukweli ni kuwa wazazi lazima wanunue baadhi ya vitabu,” aliongeza Bw Wangenye.

You can share this post!

Wafanyakazi wa kaunti wakosa ujira wa Februari

Amerika yataja Wakenya wawili magaidi sugu wa kimataifa

adminleo