• Nairobi
  • Last Updated May 4th, 2024 5:55 AM
Wanachuo wakabiliana na polisi wakipinga faini

Wanachuo wakabiliana na polisi wakipinga faini

STELLA CHERONO na MERCY KOSKEI

BEWA Kuu la Chuo Kikuu cha Egerton, Jumatatu liligeuka uwanja wa vita, wanafunzi wakikabiliana na polisi wakitaka waruhusiwe kurejea chuoni bila kulipa fidia ya Sh7,000 kwa kuharibu mali ya chuo.

Usimamizi wa chuo ulikuwa umeweka masharti kwamba kila mwanafunzi lazima alipe fedha hizo kutokana na uharibifu wa mali ya chuo mnamo Disemba 4, 2019 baada ya wanafunzi kugoma.

Wanafunzi waliopandwa na mori walipinga hatua hiyo wakisema chuo chao kinatumia kisingizio hicho kupata fedha maradufu kutoka kwao.

“Kiasi wanachotoza ni cha juu mno. Chuo kina zaidi ya wanafunzi 10,000, hiyo ikiwa na maana kwamba zaidi ya Sh70 milioni zitapatikana. Ukitathmini kiasi cha uharibifu, utagundua fedha hizo ni za juu mno,” akasema mwanafunzi mmoja kutoka chuo hicho.

Vurugu hizo zilitatiza usafiri kwenye barabara ya Njoro-Mau Narok, waendeshaji wa magari wakilazimika kuondoa mawe ambayo yalikuwa yamewekwa na wanafunzi kuziba barabara hiyo.

Usimamizi uliwaruhusu wanafunzi wa mwaka wa kwanza na wa nne pekee chuoni japo kwa masharti kwamba kila mwanafunzi lazima atie saini barua ya kukubali kugharimia uharibifu huo na kuahidi kutoshiriki ghasia tena.

Kufikia saa sita mchana hapo jana, wanafunzi tisa walikuwa wamenyakwa na polisi ambao walitumwa kutuliza ghasia hizo zilizokuwa zinaelekea kusambaa hadi miji ya Njoro na Elburgon.

Wanafunzi waliorejea chuoni walikuwa wameanza kuvamia maduka na kuwaamrisha wafanyabiashara wawape maji na chakula bila malipo.

“Utata unaendelea na serikali inafaa iingilie kati kisha iwatume wakaguzi kutathmini kiwango cha uharibifu kabla hatujaambiwa kiasi cha kulipa. Kiwango ambacho wanaitisha ni cha juu sana,” akasema mwanafunzi mwingine kwa jina Samwel Kimani.

Kwa mujibu wa mwanafunzi huyo, chuo hicho kilianzisha matumizi ya kadi maalum ya mtihani kwa wanafunzi waliomaliza kulipa karo.

Wafanyabiashara katika mji wa Njoro nao hawakuwa na budi ila kufunga biashara zao wakihofia maandamano na vurugu hizo zingewasababishia hasara kubwa.

Mfanyabiashara kwa jina Sammwel Macharia ambaye alifunga biashara yake, alisema alikuwa na matumaini ya hali kurejea kama kawaida leo.

Chuo hicho mnamo Desemba ilitishia kuahirisha shughuli za masomo kwa mwaka mmoja kwa wanafunzi wasiokamilisha karo yao, jambo lililochochea maandamano makubwa na kusababisha kufungwa kwake.

You can share this post!

Msiingize siasa katika BBI, viongozi wa kidini waonya

Miguna: Serikali yaitwa kortini Januari 21

adminleo