• Nairobi
  • Last Updated May 1st, 2024 10:08 PM
Wanafunzi wa Kidato cha Nne, Darasa la Nane na Darasa la Nne kurejea shuleni Jumatatu

Wanafunzi wa Kidato cha Nne, Darasa la Nane na Darasa la Nne kurejea shuleni Jumatatu

NA FAUSTINE NGILA

WIZARA ya Elimu imewataka wanafunzi wa Kidato cha Nne, Darasa la Nane na Darasa la Nne kurejea shuleni Jumatatu ijayo kukamilisha masomo ya muhula wa pili wa mwaka huu, yatakayoendelea kwa wiki 11.

Kwenye taarifa iliyotuma kwenye vyombo vya habari Jumanne, wizara hiyo ilifafanua kuwa ilifikia uamuzi huo kufuatia mazungumzo ya kina na washikadau husika.

Hata hivyo, Waziri wa Elimu alizitaka shule kuendelea kufuata kanuni za kuthibiti maambukizi ya virusi vya corona kama vile kuvaaa maski, kupima joto la wanafunzi na walimu, kunawa mikono na kudumisha hali ya juu ya usafi.

“Shule zote ambazo zilitumika kama vituo vya karantini vimepuliziwa dawa ya kuua viini vya corona kutayarisha madarasa kwa masomo. Walimu wote wanahimizwa kuwapa nasaha wanafunzi watakokuwa na matatizo ya mpangilio huu,” ikasema taarifa kutoka kwa wizara hiyo.

Kulingana na agizo hilo, wanafunzi hao wataenda kwa likizo ya wiki moja siku moja kabla ya Krismasi, hapo Desemba 24, 2020 na kurejea tena mwakani Januari 4, 2021 kwa muhula wa tatu.

Mitihani ya kitaifa ya KCPE na KCSE itafanyika kutoka Machi 22 hadi Machi 24, 2021 na Machi 25 hadi Aprili 4, 2021 mtawalia. Matokeo ya mtihani wa KCSE yatatangazwa hapo Mei 2021.

“Wizara ya Elimu itashirikiana na Wizara ya Afya kufuatilia miongozo na mapendekezo ya kufungua shule ili kutambua ni lini wanafunzi wote waliosalia watarejea darasani,” ikasema taarifa hiyo.

 

 

You can share this post!

KRU kuandaa mchujo kwa ajili ya vikosi vya raga kupanda na...

Muungano wa maendeleo ya wanawake walaani ghasia za...