Habari

Aladwa awarai wanachama wa ODM wasusie maandamano Saba Saba

Na KEVIN CHERUIYOT July 6th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

BAADHI ya viongozi wa ODM katika Kaunti ya Nairobi wamewataka wafuasi wao wasishiriki maandamano ya Saba Saba ambayo yanapangwa kufanyika hapo kesho.

Wakiongea Nairobi Jumapili, viongozi hao walisema wao ni sehemu ya Serikali Jumuishi na njia ya kusaka suluhu kwa changamoto za nchi ni kupitia mazungumzo badala ya maandamano.

Mbunge wa Makadara, George Aladwa, ambaye pia ni Mwenyekiti wa ODM Kaunti ya Nairobi alitoa wito wa umoja kati ya viongozi na akawataka polisi wahakikishe kuwa waandamanaji hawaharibu mali.

“Tunasema hakuna mwanachama wetu ambaye atatumika kuzua ghasia jijini na taifa lote. Sote tuko katika Serikali Jumuishi na tunasema kuwa hatutaingia barabarani kwa ajili ya maandamano ya Saba Saba,” akasema Bw Aladwa.

Kauli yake ilijiri wakati ambapo wanaharakati wa kibinadamu wametoa wito wa kuandaliwa kwa maandamano kupinga kutoweka kwa watu kwa njia tatanishi na pia mauaji ya kiholela mikononi mwa polisi.

Mbunge huyo aliwataka Waziri wa Usalama wa Ndani, Kipchumba Murkomen na Katibu wa wizara hiyo, Dkt Raymond Omollo kuwalinda Wakenya dhidi ya maandamano yoyote ambayo yanatishia amani ya nchi.

Aidha waliwaonya wale ambao wamekuwa wakimshutumu Dkt Omollo kutokana na utendakazi wake, akisema katibu huyo ataendelea kuhudumu serikalini hadi 2027.

“Katibu Omollo anafaa aruhusiwe kuendelea na kazi yake bila kuingiliwa. Wale ambao wana malalamishi dhidi yake wayafikishe katika afisi yake jumba la Harambee,” akasema.

Vilevile Bw Aladwa na viongozi alioandamana nao walisema Kenya ni nchi ambako uhuru wa vyombo vya habari unaheshimiwa katika kutia mizani utendakazi wa upinzani na serikalini.

“Ni vyema iwapo vyombo vya habari vitamakinikia amani hata vikishutumu viongozi wa kisiasa. Kama utendakazi wangu ni duni, chombo cha habari kina uhuru wa kunimulika. Tunahitaji amani kuelekea uchaguzi wa 2027,” akasema.

Kuhusu uongozi wa ODM alipuuza mrengo wa Katibu Mkuu wa ODM Edwin Sifuna akisema wanaunga mkono ule wa Dkt Oburu Oginga.