Zaheer kuhojiwa, Arati akijitetea kuhusu ghasia za Keumbu
GHASIA za Ijumaa dhidi ya msafara wa Linda Mwananchi katika Kaunti ya Kisii ambapo mtu mmoja aliuawa na wengine kadhaa kujeruhiwa zinaonyesha jinsi ushindani wa kisiasa unavyoendelea kuzua uhasama huku uchaguzi mkuu wa 2027 ukikaribia.
Idara ya polisi jana ilithibitisha kuwa maafisa wa usalama wamewakamata washukiwa saba na kuwahakikishia Wakenya kuwa msako wa kuwatafuta washukiwa wengine unaendelea.
Tukio hilo limethibitisha kuwa baadhi ya viongozi wakuu wa kisiasa katika eneo la Gusii wanahusika katika kueneza na kufadhili uhuni wa kisiasa ili kusambaratisha mikutano ya wapinzani wao.
Mbunge mmoja anayehudumu muhula wa kwanza akishirikiana na kiongozi mmoja wa ngazi ya kaunti wanahusishwa na kufadhili ghasia hizo zilizotokea eneo la Keumbu.
Inadaiwa viongozi hao wawili waliwanunulia vijana mipini ya majembe, mapanga na silaha nyingine ili kuvamia mikutano ya Linda Mwananchi.
Hapo jana, maafisa kutoka Idara ya Upelelezi (DCI) mjini Kisii walisema kuwa wamemwamrisha Mbunge wa Nyaribari Chache Zaheer Jhanda afike mbele yao ili ahojiwe kuhusu ghasia hizo zilizosababisha kifo cha mtu mmoja.
“Mbunge Zaheer Jhanda, ameagizwa kufika katika afisi za DCI, Kaunti ya Kisii leo asubuhi kuhusiana na uchunguzi unaoendelea,” ikasema taarifa ya Idara ya Polisi ikisisitiza kuwa wote waliovamia msafara wa Linda Wananchi watanyakwa na kufikishwa kortini.
Vincent Osiemo ‘Mapinduzi’ aliaga dunia jana hospitalini. Alikufa kutokana na majeraha ya kuanguka kutoka kwenye gari lililokuwa likiendeshwa kwa kasi huku madereva wakikwepa mawe yaliyokuwa yakirushwa Keumbu. Marehemu alikuwa alikuwa katika kikosi cha wanahabari wanaofanyia kazi Linda Mwananchi.
Taarifa hiyo ilitolewa baada ya wananchi kuonyesha hasira baada ya kusambaa kwa video zilizoonyesha polisi wakitembea sako kwa bako na watu waliodhaniwa kuwa wahuni waliokuwa wakiurushia mawe msafara wa Linda Mwananchi.
Wabunge Clive Gesairo (Kitutu Masaba) na mwenzake wa Bomachoge Borabu, Obadiah Barongo, waliotangaza kifo cha kijana huyo, walishutumu vyombo vya usalama kwa kutoa silaha kwa makundi ya wahuni wa kisiasa.
Wanasiasa hao wawili walithibitisha kuwa watu 20 walijeruhiwa kutokana na ghasia za eneo la Keumbu.
Gavana wa Kisii, Simba Arati, naye amepinga madai kuwa alihusika kwa kufadhili wahuni dhidi ya viongozi wa Linda Mwananchi. Bila kutoa ushahidi wowote, gavana huyo alidai kuwa baada ya viongozi wa upinzani kumaliza mikutano yao, waliwaachilia “wahuni wao” waliowaleta Kisii kuwashambulia wananchi wasio na hatia, na hivyo kuwalazimu wakazi kujilinda.
“Niliwaambia wafuasi wangu wasiingilie mkutano wa Linda Mwananchi. Baada ya kumaliza mikutano yao kwa amani, waliwaachilia wahuni wao waliowaleta Kisii na kuwalazimisha wananchi wajilinde dhidi ya wahuni hao,” akasema Bw Arati mjini Ogembo.
“Nawauliza watu wa Ogembo, mnaweza kutazama watu waje hapa waanzishe fujo bila kujitetea?” akauliza.
Video zilionyesha wavamizi wakirusha mawe kwenye magari yaliyokuwa katika msafara wa viongozi wa upinzani.
Madereva walikimbia kwa hofu huku baadhi ya wafuasi wakidondoka kutoka kwenye magari na kujeruhiwa vibaya.
Kwenye video hiyo hakuna ushahidi unaoonyesha kuwa kulikuwa na makundi mawili yaliyokuwa yakipigana kama ilivyodaiwa na gavana pamoja na baadhi ya maafisa wa usalama wa Kisii.
Wavamizi hao walionekana kuwa wamejipanga vizuri na walikuwa na silaha tayari kutekeleza uhalifu huo ulionekana ulipangwa mapema.
Aliyekuwa Jaji Mkuu David Maraga, ambaye alijiunga na timu ya Linda Mwananchi Ijumaa, gari lake liliharibiwa katika vurugu hizo za kurushiana mawe.
Naibu Kiongozi wa Chama cha Jubilee Dkt Fred Matiang’i, ambaye ngome yake ya kisiasa ni Kisii, alitaka Kamanda wa Polisi wa Kaunti ya Kisii afutwe kazi kutokana na kisa hicho.
Mweka Hazina wa Kitaifa wa ODM Timothy Bosire, ambaye anatoka Nyamira, alitaja ghasia hizo kuwa mbinu za kisiasa zilizopitwa na wakati akizua maswali kuhusu mbona msafara huo ulishambuliwa Keumbu ilhali ulikuwa umepita maeneo mbalimbali kwa amani.