Ruto atua ngome ya Kalonzo na minofu uchaguzi ukikaribia
RAIS William Ruto amewataka viongozi wa upinzani kutafuta hoja bora za kupinga ajenda yake ya maendeleo badala ya kuwagawanya Wakenya kwa misingi ya ukabila.
Rais alisema hayo jana alipofanya ziara katika Kaunti ya Machakos, ngome ya kisiasa ya kiongozi wa Wiper Patriotic Front Kalonzo Musyoka, huku akijaribu kuvutia wakazi wa Ukambani kuelekea uchaguzi wa 2027.
Rais pia alishutumu upinzani kwa kukosa ajenda thabiti ya kisiasa na kudai baadhi yao wanafanya kazi kwa niaba ya viongozi wengine.
“Ingawa umeajiriwa na umekubali kuwa kikaragosi, usijiaibishe. Mnaenda kusema tatizo kubwa la mpango wa nyumba za bei nafuu ni kuku kushindwa kupanda ngazi. Huo ni ujinga. Tafuteni hoja bora,” alisema Rais Ruto katika mikutano mitatu aliyoandaa Machakos.
Aliongeza: “Mnaendelea pia kusema mtavunja SHA. Tafuteni hoja bora ya kuwasilisha kwa Wakenya.” Rais alisema wakati umefika ambapo Wakenya wanapaswa kuwahukumu viongozi kwa rekodi zao za uongozi, mipango na maono badala ya matusi na kauli za kisiasa.
“Wakenya hawana haja na wale wanaowagawanya kwa kuwaita wengine binamu, wengine wasaliti na wengine maadui. Kenya inahitaji umoja. Sisi sote ni ndugu,” alisema katika mkutano Kimutwa Township.