BATUK: Wabunge wadai Kenya haijaingia katika makubaliano na Uingereza
Wabunge wamesisitiza kuwa hakuna makubaliano mapya yaliyofikiwa kati ya Kenya na Uingereza kuhusu mkataba wa ushirikiano wa kijeshi na Kenya (BATUK).
Kauli hiyo inajiri baada ya Uingereza kusema kuwa kumekuwa na maendeleo makubwa katika kutekeleza baadhi ya mapendekezo yaliyotolewa na Kamati ya Bunge kuhusu Ulinzi.
Uingereza ilisema maafisa wake wakuu walikutana na maafisa wa serikali ya Kenya, wabunge na wajumbe wa Kamati ya Ulinzi na Masuala ya Kigeni Juni kujadili hatua iliyofikiwa.
“Maafisa wakuu wa Uingereza walikutana na maafisa wa Serikali ya Kenya, wabunge na wajumbe wa Kamati ya Ulinzi na Masuala ya Kigeni mwezi Juni kujadili maendeleo yaliyofikiwa hadi sasa,” ilisema taarifa hiyo.
Uingereza pia ilisema taratibu za pamoja za kushughulikia mabomu na vilipuzi ambavyo havijalipuka zimekamilishwa.
Miongoni mwa masuala mengine yaliyoshughulikiwa ni mahitaji ya ulinzi wa mazingira na matumizi ya ardhi, ambayo yamewasilishwa kwa mamlaka husika.
Uingereza pia ilisema imeweka hatua mpya za kuzuia unyanyasaji wa kingono.
Hata hivyo, Kamati ya Bunge kuhusu Ulinzi iliambia Bunge Jumanne kuwa mkataba huo bado haujaidhinishwa.
Mwenyekiti wa kamati hiyo, Nelson Koech, alisema makubaliano hayo hayawezi kuanza kutumika hadi masharti yaliyowekwa na Kenya yatimizwe.
Bunge linataka vifungu vya 6(5) na 23 virekebishwe ili mauaji yawe chini ya mamlaka ya mahakama za Kenya.
Wabunge pia wanataka BATUK iwe na mpango wa uwajibikaji kwa jamii unaohusisha maeneo inayofanyia shughuli zake.
Bw Koech alisema kamati haitakubali mkataba unaokiuka Katiba au kudhalilisha Wakenya.
Alisema kujumuishwa kwa mauaji katika vifungu vinavyopendekezwa kutaimarisha uwajibikaji na kuhakikisha wahalifu wa makosa hayo makubwa wanawajibishwa nchini.
Mbunge wa Laikipia wa Kike Jane Kagiri aliunga mkono msimamo huo, akisema mtu yeyote anayefanya uhalifu nchini Kenya anapaswa kufikishwa mbele ya mahakama za Kenya.
Kwa sasa, mkataba huo unaacha makosa kadhaa makubwa chini ya mamlaka ya Kenya, lakini mauaji hayajajumuishwa katika orodha hiyo.
Hali hiyo imeibua wasiwasi kwamba Uingereza inaweza kudai mamlaka ya kushughulikia kesi za mauaji yanayohusisha wanajeshi wake.
Bw Koech alisema masharti ya kamati bado hayajatimizwa licha ya serikali kutangaza kuanza tena kwa mafunzo ya pamoja ya kijeshi kati ya Kenya na Uingereza katika kituo cha BATUK, Laikipia.
Alisema mazungumzo na kubadilishana mawasiliano kumeendelea, lakini Uingereza bado haijatoa ahadi ya kutosha kuhusu madai ya Kenya.
BATUK imekuwa ikifanya shughuli nchini Kenya chini ya Mkataba wa Ushirikiano wa Ulinzi kati ya Kenya na Uingereza uliopitishwa mwaka 2016.
Mkataba mpya uliwasilishwa Bungeni mwaka 2021 baada ya muda wa mkataba wa awali wa miaka mitano kuisha.
Hata hivyo, Bunge la 12 lilimaliza muda wake kabla ya kuidhinisha mkataba huo.
Mkataba huo uliwasilishwa tena kwa Bunge la 13 mwezi Novemba 2022.
Baada ya kushirikisha wananchi, kamati ilipendekeza uidhinishwe kwa masharti kwamba vifungu vya 6(5) na 23 virekebishwe kabla ya kuanza kutumika.