Habari

Hofu kijijini watoto 10 wakijitia kitanzi

Na NA MERCY KOSKEI August 9th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

HOFU imetanda katika eneo la Ndabibi Central, Naivasha, baada ya watoto wasiopungua 10 kujitia kitanzi katika kipindi cha mwaka mmoja.

Wakazi wanasema visa hivyo vimeacha familia zikijiuliza kinachowasukuma watoto wadogo kujiua.

Miongoni mwa waliofariki ni Cynthia Muthoni, mwanafunzi wa Gredi ya Sita.

Asubuhi ya Juni 6, alionekana kuwa sawa nyumbani kwao.

Rachael Wahu Kariuki na binti yake walikuwa wameenda mtoni kufua nguo kabla ya kurejea nyumbani.

Mchana, Wahu alimwacha Muthoni akiosha vyombo na kumuagiza apike chakula kabla ya yeye kurejea kazini.

Karibu saa tisa alasiri, mama huyo alirudi nyumbani na kumpata binti yake akiwa katika hali nzuri.

Aliondoka tena baada ya kuitwa shuleni. Muda mfupi baadaye, majirani wawili walifika kwa pikipiki na kumuomba awafuate.

Walimpeleka kwa jirani, ambapo Wahu aliambiwa binti yake alikuwa amefariki baada ya kujitia kitanzi.

Dada yake ndiye aliyegundua na kuwaarifu majirani.

“Nilimwacha akiwa na furaha. Hakuwa amefanya kosa lolote na hatukuwa tumegombana. Sijui ni nini kilimfanya ajitie kitanzi,” alisema Wahu kwa machozi.

Mama huyo alisema Muthoni alikuwa amewahi kuugua ugonjwa wa figo.

Dawa alizokuwa akitumia zilifanya mwili wake uvimbe na akaanza kuogopa kuchekwa na wanafunzi wenzake.

Alikuwa pia amekataa kurejea shuleni na alitaka kujiunga na mafunzo ya ufundi.

Kilomita chache kutoka hapo, familia ya Kiragu Mochogua ilikuwa ikiomboleza kifo cha binti yao wa miaka 16, Jane Wanjiru.

Jane alikuwa ameenda kutafuta kuni lakini hakurudi nyumbani.Baba yake alimfuata msituni baada ya kuona nyayo zake.Huko ndiko alipompata binti yake akiwa amefariki.

Mama yake, Phyllis Wambui, alisema Jane alikuwa akisumbuliwa na matatizo ya afya na aliacha shule akiwa Darasa la Tano.

Dada yake mdogo pia aliacha shule akiwa Darasa la Tatu ili kumhudumia.

Familia ilikuwa imeanza kupanga kumrudisha Jane shuleni baada ya afya yake kuimarika.

Lakini alifariki kabla ya mpango huo kutimia.

Kifo cha Beth Nyaguthie Juma, mwanafunzi wa Gredi ya Sita, pia kimeongeza majonzi katika eneo hilo.

Kaka yake, Peter Chege Juma, alisema alipokea simu ya dharura kutoka kwa majirani na kukimbia nyumbani.

Alisema kifo cha dada yake kilimvunja moyo kiasi kwamba aliondoka nyumbani kwao na kukodisha nyumba.

“Mama yetu alifariki 2024. Dada yangu alikuwa kitindamimba. Kifo chake kilituacha na maumivu makubwa,” alisema.

Chifu msaidizi wa Ndabibi Central, Aseth Kariuki, alisema visa hivyo vinazidi kuwa vya kutisha.

Alisema watoto wenye umri wa kati ya miaka 12 na 15 ndio walioathirika zaidi.

“Mwaka huu pekee, tumewazika watoto watano waliofariki baada ya kujitia kitanzi Ndabibi. Tulipofuatilia visa hivyo, wazazi na walimu walisema hawakuona ishara zozote za hatari,” alisema.

Mercy Wangui Mburu, mwalimu na mhudumu wa kulinda watoto, alisema angalau watoto 10 wamefariki kwa kujitia kitanzi katika eneo hilo tangu Juni mwaka uliopita.

Watoto wengine saba wamejaribu kujiua.Wengi wa walioathirika wana umri wa miaka 12 hadi 17.

Wangui alisema wahudumu wa jamii wamelemewa na visa hivyo.

“Tunahitaji washauri wa kitaalamu. Hata kama watakaa hapa kwa miezi miwili. Tunataka kuelewa watoto hawa wanapitia nini kwa sababu wanateseka kimya kimya,” alisema.

Alitaka serikali za kitaifa na kaunti kuingilia kati na kuimarisha huduma za afya ya akili katika shule, makanisa na familia.

Mtaalamu wa ushauri nasaha Meshack Ondieki alisema wazazi wanapaswa kuwasikiliza watoto wao na kuzingatia mabadiliko katika tabia zao.

Alisema ishara za kuangaliwa ni pamoja na kujitenga na familia, kushuka kwa matokeo shuleni, kupoteza hamu ya shughuli walizopenda na kubadilika kwa uhusiano wao na wenzao.

Pia alisema kukosa hamu ya kula, uchovu wa mara kwa mara, kupuuza usafi wa kibinafsi na kukataa kushiriki shughuli za kawaida vinaweza kuwa ishara kwamba mtoto anapitia matatizo ya kihisia.

Alisema mabadiliko hayo hayafai kupuuzwa kama tabia za kawaida za ujana, hasa yanapotokea kwa pamoja.

Kulingana na takwimu za Kaunti ya Nakuru zilizotajwa na wataalamu wa afya ya akili, zaidi ya visa 400 vinavyohusiana na kujiua viliripotiwa kati ya Januari 2020 na Aprili 2025.

Takwimu hizo zinaonyesha ukubwa wa changamoto inayokabili watoto na vijana katika eneo hilo.