Habari za Kitaifa

Mlipuko wa lori la mafuta, watatu wafariki, 23 wajeruhiwa, 11 mahututi

Na TITUS OMINDE September 18th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

Watu watatu walifariki na wengine 23 kujeruhiwa, 11 kati yao wakalazwa katika chumba cha wagonjwa mahututi (ICU), baada ya lori la mafuta kulipuka katika eneo la Juakali, Turbo, kando ya barabara kuu ya Eldoret-Webuye.

Mkasa huo ulitokea baada ya umati wa wakazi kufurika katika eneo hilo kuchota mafuta yaliyokuwa yakivuja kutoka kwa lori lililokuwa limepata ajali.

Walioshuhudia walisema lori hilo lilipinduka na muda mfupi baadaye likalipuka, na kusababisha moto mkubwa uliowapata watu waliokuwa wakichota mafuta.

Waathiriwa walichomeka vibaya kiasi cha kutotambulika, huku majeruhi wakikimbizwa katika Hospitali ya Mafunzo na Rufaa ya Moi (MTRH), Eldoret.

Mkurugenzi wa Matibabu wa MTRH, Dk Andrew Wandera, alisema hospitali hiyo imepokea majeruhi 23 pamoja na miili miwili kabla ya manusura mmoja kufariki baadaye.

“Tulipokea majeruhi 23 pamoja na miili miwili. Mwingine alifariki alipokuwa akipatiwa matibabu katika ICU,” alisema Dkt Wandera.

Alisema majeruhi wengi walikuwa na majeraha makubwa ya kuchomeka, baadhi wakiungua zaidi ya asilimia 70 ya miili yao.

Juhudi za waokoaji na maafisa wa kukabiliana na majanga ziliendelea katika eneo la mkasa huku baadhi ya miili ikidaiwa kunaswa chini ya mabaki ya lori hilo.

Kamanda wa Polisi wa Kaunti ya Uasin Gishu, Wilberforce Sicharani, alithibitisha mkasa huo na kuutaja kuwa wa kuhuzunisha.

“Hii imekuwa ajali mbaya sana. Watu wamepoteza maisha kwa njia ya uchungu mkubwa,” alisema.N