Habari

Cofek yakimbia kortini kuzima vipengee tata kwenye Mswada wa Fedha 2026

Na JOSEPH WANGUI June 17th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

SHIRIKISHO la Watumiaji bidhaa nchini (Cofek) limewasilisha kesi katika Mahakama Kuu likitaka kuondolewa kwa baadhi ya vipengele vya Mswada wa Fedha wa 2026, likidai vinaweza kuongeza gharama ya maisha na kuhatarisha haki za walipa ushuru.

Katika kesi iliyowasilishwa katika Kitengo cha Katiba na Haki za Kibinadamu, Cofek inataka mahakama izuie utekelezaji wa vipengele hivyo iwapo Bunge litavipitisha kuwa sheria.

Shirikisho hilo linaonya kuwa kuondolewa kwa msamaha wa Ushuru wa Ongezeko la Thamani (VAT) kwa baadhi ya bidhaa muhimu kutasababisha kupanda kwa bei za vyakula, bidhaa za afya, pembejeo za kilimo na vifaa vya elimu, huku mzigo huo ukibebwa na watumiaji bidhaa.

Aidha, Cofek inaeleza kuwa mapendekezo ya kupanua nguvu za Mamlaka ya Ushuru Kenya (KRA) inaweza kuruhusu utozaji wa ushuru bila taratibu za haki, ikiwemo kuondoa nafasi ya kusikilizwa.