Habari Mseto

Maraga: Kuondoa Ruto hakutoshi, lazima tung’oe mizizi inayoleta mafidhuli uongozini

Na JOSEPH KINUTHIA, NDUBI MOTURI June 17th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MGOMBEA urais wa chama cha United Green Movement (UGM), David Maraga, ametoa wito kwa vyama vya upinzani kuungana kwa misingi ya maadili, utawala wa sheria na kuheshimu Katiba, akisema Kenya inahitaji mwanzo mpya ili kukabili ufisadi, kudorora kwa uchumi na kuporomoka kwa taasisi za umma.

Akizungumza katika hotuba yake ya Hali ya Taifa aliyotoa akiwa Ufungamano House, Nairobi, baada ya kukamilisha ziara aliyoita ‘Ukatiba Caravan’ katika kaunti 43, aliyekuwa Jaji Mkuu alisema uchaguzi mkuu wa 2027 utakuwa wa kuamua hatima ya nchi.

“Ninaamini katika umoja wa upinzani, lakini umoja huo lazima ujengwe kwa misingi ya maadili na si tamaa ya madaraka. Lazima tuungane chini ya utawala wa sheria ili kuhakikisha hakuna kiongozi atakayetumia mamlaka vibaya kupora rasilimali za umma, kuua watoto wetu au kuzima sauti za wakosoaji,” alisema.

Bw Maraga alisema safari yake ya kuzunguka nchi ilimfanya ashuhudie malalamishi mengi kutoka kwa wananchi kuhusu ufisadi uliokithiri, ukosefu wa ajira, gharama ya juu ya maisha na kuzorota kwa huduma za afya na elimu.

Alisema Wakenya walionyesha kuwa bado wana matumaini licha ya changamoto wanazopitia, lakini walilalamikia kupuuzwa kwa utawala wa sheria, kuingiliwa kwa taasisi za umma na kuendelea kwa ufisadi.

Kwa mujibu wake, viongozi wameisaliti ndoto ya waanzilishi wa taifa kwa kugeuza serikali kuwa njia ya kujinufaisha wao wenyewe, familia zao na washirika wao.

Bw Maraga alimshutumu Rais William Ruto kwa kile alichodai kuwa kuendeleza ufisadi na kuongeza deni la taifa kupita kiasi, akisema karibu nusu ya bajeti ya serikali sasa inaelekezwa kulipa madeni.

Katika mpango wake wa kuongoza Kenya, Bw Maraga alisema serikali yake itajikita katika nguzo tatu za kurekebisha, kurejesha na kujenga upya taifa.

Aliahidi kuimarisha taasisi za umma, kuheshimu Katiba, kukomesha mauaji ya kiholela na kukabiliana vikali na ufisadi.

“Nitahakikisha Katiba ndiyo mwongozo mkuu wa serikali yangu. Hakutakuwa na aliye juu ya sheria,” alisema.

Aidha aliahidi kufufua uchumi kupitia kilimo, viwanda na ubunifu wa teknolojia huku akiwapa vijana nafasi zaidi za ajira na matumizi ya Akili Unde (AI).

Maraga alisema hajawahi kuhusishwa na kashfa yoyote ya ufisadi na yuko tayari kutangaza mali yake hadharani, akiwataka wagombeaji wengine wa urais kufanya vivyo hivyo.

“Kuondoa Rais Ruto pekee hakutoshi. Lazima tubadili mfumo mzima wa uongozi. Serikali ijayo isiwe mchezo wa kubadilishana viti huku watu walewale wakiendelea kujinufaisha,” alisema.

Katika mkutano huo, viongozi mbalimbali wa upinzani akiwemo Martha Karua, Caleb Amisi, Wilberforce Oundo na Caroli Omondi walisisitiza umuhimu wa kuungana ili kuondoa nchi katika matatizo ya sasa na kujenga uongozi unaozingatia uwajibikaji na maslahi ya wananchi.