Habari

Familia zalalamikia kuzuiwa kuchukua miili ya wahanga wa Utumishi Girls

Na NA LELETI JASSOR June 8th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

WAZAZI na jamaa za wasichana 16 walioangamia kwenye mkasa wa moto katika Shule ya Wasichana ya Utumishi sasa watasubiri hadi Juni 17, 2026 ili kupewa miili ya waathiriwa baada ya ibada ya pamoja.
Mnamo Jumamosi, wazazi hao waliondoka makafani ya Naivasha wakiwa wamefadhaika baada ya kuzuiwa kuchukua miili ya watoto wao.
Tahuriki na huzuni ilitanda katika makafani hayo baada ya matokeo ya uchunguzi wa DNA kutambua miili ya watoto hao.
Baadhi ya wazazi walikerwa wakisema Juni 17 ni mbali na wanataka wapewe miili ya watoto wao waizike kisha waendelee na maisha yao.
“Tulikuja hapo tukiwa na matumaini ya kuambiwa siku ya kuchukua miili kwa mazishi. Tulipofika tulipewa maelezo ambayo hayaridhishi na tukaambiwa miili itatolewa tu mnamo Juni 17,” akasema John Muiruri babake marehemu Nicole Mitche Muiruri.
Alishangaa kwa nini bado walikuwa wakizuiwa kuchukua miili ilhali kiini cha moto huo kishajulikana, utambuzi wa DNA umekamilishwa pamoja na masuala mengine yanayohusiana na kisa hicho.
Mchungaji Dan Parisoi, ambaye ni jamaa wa marehemu Purity Naisula, mwanafunzi wa kidato cha nne, alisema kusubiri ni kuongezea tu familia huzuni.
“Kando na kutuumiza kisaikolojia pia tunagharimika kifedha. Pesa ambazo zinatolewa na serikali ni kidogo na hazigharimii mahitaji,” akasema Mchungaji Parisoi.
Naibu Kamishina wa Gilgil Stanley Langat Mutai alisema mashauriano yanaendelea kuhusu malalamishi ya baadhi ya wazazi kuwa Juni 17 ni mbali na hawawezi kusubiri hadi wakati huo kuchukua miili ya watoto.
“Tunawaomba wazazi ambao watoto wao wapo katika makafani haya watie subira kwa sababu tunashauriana kuona iwapo tarahe hiyo inaweza kurejeshwa nyuma,” akasema Bw Mutai.