Habari za Kaunti

Mabaharia kuepuka kukamatwa ovyo mpakani baada ya Ruto kukutana na Suluhu

Na KALUME KAZUNGU May 7th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MABAHARIA na wavuvi nchini wanatarajia kufaidika baada ya serikali za Kenya na Tanzania kutia saini Mkataba wa Makubaliano (MoU) kuhusu Utambuzi wa Vyeti vya Baharini na Usimamizi wa Sekta ya Usafiri wa Majini kati ya nchi hizo mbili.

Hatua hii inatarajiwa kupunguza mizozo ambayo imekuwa ikishuhudiwa miaka ya nyuma wakati wavuvi wanapovuka mipaka baharini, hata kwa mita chache, ambapo huishia kukamatwa na vifaa vyao vya uvuvi kutwaliwa.

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Ubaharia nchini (KMA) Omae Nyarandi, alishiriki katika utiaji saini wa makubaliano yaliyofanyika katika Ikulu ya Dar es Salaam, mbele ya Rais William Ruto, na Rais Samia Suluhu Hassan wa Tanzania.

Kulingana nao, makubaliano haya ni muhimu na yanaonyesha dhamira endelevu ya nchi zote mbili kuimarisha ushirikiano, kuboresha usalama na viwango vya sekta ya baharini, pamoja na kukuza usimamizi bora wa sekta ya usafiri wa majini katika ukanda huu.

Mbali na wavuvi, makubaliano hayo yanaweza pia kupunguza vikwazo ambavyo kwa muda mrefu vimekuwa vikichelewesha shughuli za usafiri wa majini wa kuvuka mipaka, huku pia yakiboresha usalama na viwango vya kitaaluma kupitia ulinganifu wa vyeti.

Usafiri wa majini kati ya Kenya na Tanzania huhusisha zaidi uchukuzi wa mizigo bandarini.

“Kwa kusaini makubaliano haya, nchi hizi mbili zinalenga kuboresha ufanisi katika huduma za usafiri wa abiria majini, kukuza biashara ya ukanda wa pwani, na kuchochea ukuaji wa uchumi katika eneo la Afrika Mashariki,” alisema Bw Nyarandi.

Makubaliano hayo yanatarajiwa pia kufungua fursa za ajira kwa wataalamu wa sekta ya baharini katika nchi zote mbili, pamoja na kuimarisha uwezo wa kiufundi kupitia kubadilishana ujuzi na mipango ya mafunzo ya pamoja.

Maafisa walibainisha kuwa, makubaliano hayo pia yataimarisha ushirikiano katika maeneo muhimu kama vile maendeleo ya bandari, usalama na ulinzi wa baharini, pamoja na uhifadhi wa mazingira, hasa katika kushughulikia uchafuzi wa bahari na matumizi endelevu ya rasilimali za bahari.

Sekta ya baharini ni nguzo muhimu ya mageuzi ya kiuchumi katika ukanda huu. Kuimarisha ushirikiano kama huo ni muhimu katika kufungua uwezo wake kamili.

Makubaliano hayo pia yanaashiria msukumo mpya wa kuimarisha ushirikiano wa kikanda, sambamba na juhudi zinazoendelea chini ya mfumo wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) za kulinganisha sera na kuboresha miundombinu ya mawasiliano.

Kwa Tanzania, makubaliano haya yanaonyesha dhamira ya kujenga sekta ya baharini iliyo endelevu na shirikishi, huku kwa Kenya yakithibitisha juhudi za kujipanga kama kitovu cha usafirishaji na usambazaji katika ukanda huu.