Habari za Kitaifa

Mpango wasukwa kuleta shirikisho jipya la wafanyakazi kupunguza ushawishi wa Cotu

Na KEVIN CHERUIYOT May 7th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

JUHUDI za kuanzisha muungano mbadala wa wafanyakazi kwa lengo la kudhoofisha Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi (COTU) Kenya chini ya Katibu Mkuu Francis Atwoli zimeanza kupata nguvu nchini.

Wanaosukuma mpango huo ni pamoja na aliyekuwa naibu rais na kiongozi wa chama cha Democracy for the Citizens Party (DCP), Rigathi Gachagua, pamoja na aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usimamizi wa Usalama wa Kibinafsi, Fazul Mohamed.

COTU, ambao ni muungano mkuu unaounganisha vyama vya wafanyakazi nchini na wanachama takriban 4.8 milioni kupitia mashirika mbalimbali, ilianzishwa 1965 baada ya kuvunjwa kwa lililokuwa Shirikisho la Leba na Wafanyakazi Waafrika Kenya.

Ingawa COTU ilianzishwa kutetea haki za wafanyakazi nchini na kimataifa, baadhi ya sauti zinasema Katibu Mkuu ameacha wajibu wake na kwamba taasisi mpya inahitajika.

Gachagua amedai Atwoli amehudumu kwa muda mrefu baada ya kuchaguliwa tena kwa muhula wa sita, akisema uongozi wa wafanyakazi unahitaji damu mpya.

Alimkosoa pia kwa kujihusisha zaidi na siasa za uchaguzi wa 2027 badala ya maslahi ya wafanyakazi.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa ripoti kuhusu soko la ajira na ustawi wa wafanyakazi 2026, Gachagua alisema yuko tayari kusaidia kuanzishwa kwa shirikisho mbadala la wafanyakazi.

“Ni wakati wa kuwa na chombo kingine cha wafanyakazi ili wawe na chaguo,” alisema.

Kwa upande wake, Fazul Mohamed aliunga mkono wazo hilo akisema COTU inahitaji kurekebishwa ili kuhudumia wanachama wake vyema zaidi.

Hata hivyo, COTU ilipinga kauli hizo, ikimtetea Atwoli ikisema amefanikisha mishahara na maslahi ya wafanyakazi.

Naibu Katibu Mkuu Benson Okwaro alisema Gachagua hana mamlaka ya kuzungumzia masuala ya wafanyakazi na akamtaka kuanzisha chama chake badala ya kuvuruga vyama vilivyopo.

Alisisitiza kuwa COTU ni taasisi ya muda mrefu kuliko Gachagua na itaendelea kudumu licha ya “siasa za muda mfupi.”