Habari za Kaunti

Tabasamu kwa makuli bandarini mkataba mpya ukitiwa saini kuwaongeza mishahara

Na ANTHONY KITIMO June 2nd, 2026 Kusoma ni dakika: 1

CHAMA cha Wafanyakazi wa Bandari (DWU) kimesaini Mkataba mpya wa Makubaliano ya Pamoja (CBA) na Mamlaka ya Bandari nchini (KPA), hatua inayomaliza zaidi ya miaka miwili ya mazungumzo kuhusu mishahara na marupurupu ya wafanyakazi katika Bandari ya Mombasa.

Mkataba huo ambao utafaidi zaidi ya wafanyakazi 5,000 unaohusu kipindi cha mwaka 2024 hadi 2027 umeanzisha viwango vipya vya mishahara ya msingi kwa wafanyakazi katika makundi mbalimbali ya kazi, kuongeza marupurupu ya usafiri na kulipa madeni ya nyongeza ya mishahara yatakayorejeshwa nyuma kuanzia mwaka 2024.

Katibu Mkuu wa Chama cha Wafanyakazi wa Bandari, Bw Sulman Owuor, alisema makubaliano hayo yanalenga kuboresha maslahi ya wafanyakazi huku yakidumisha utulivu katika shughuli za bandari.

Kwa mujibu wa chama hicho, wafanyakazi walio katika Daraja la 8 la KPA watapata mshahara wa msingi wa kati ya Sh92,975 na Sh127,130, huku wale wa Daraja la 9 wakilipwa kati ya Sh78,635 na Sh98,375. Wafanyakazi wa Daraja la 10 watapata mshahara wa kati ya Sh53,715 na Sh83,975.

Pande hizo mbili pia zilikubaliana kuendelea na mfumo wa sasa wa marupurupu ya nyumba, lakini zikapandisha viwango vya marupurupu ya usafiri.

Wafanyakazi wa Daraja la 8 watapokea marupurupu ya usafiri ya Sh30,000 kwa mwezi, wale wa Daraja la 9 watapata Sh20,000, huku wafanyakazi wa Daraja la 10 wakipokea Sh15,000.

Chama hicho pia kilisema kuwa madeni ya mishahara yaliyokusanywa kuanzia mwaka 2024 yatalipwa mara tu mchakato wa utekelezaji wa makubaliano hayo utakapokamilika.