Wavuvi wapewa chombo cha kuvutia samaki baharini kwa teknolojia ya kisasa
SEKTA ya uvuvi Pwani imepigwa jeki baada ya wavuvi kupokezwa vifaa vya teknolojia ya kisasa vitakavyowasaidia kuongeza pato lao la samaki baharini.
Vifaa hivyo, ikiwemo vidubwasha vyenye uwezo wa kuwavutia samaki mahali pamoja ili iwe rahisi kwa wavuvi kuwapata, vinalenga kuwapunguzia gharama.
Kufikia sasa wavuvi wa kaunti za Lamu na Kwale tayari wamepokezwa vifaa hivyo vya vinavyosambazwa chini ya ufadhili wa Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO).
Wavuvi wa kaunti hizo pia wamepokezwa majokofu ya kuhifadhia samaki.
Afisa Mwakilishi wa FAO, Dkt Joseph Othieno, alisema vifaa hivyo pia vinalenga kuhakikisha wanatekeleza uvuvi endelevu ambao ni salama kwa mazingira.
Gavana wa Lamu, Bw Issa Timamy, alisema teknolojia hiyo ni mwamko mpya kwa sekta ya uvuvi inayopitia changamoto tele.
Bw Lali Shee, ambaye amekuwa akivua samaki kwa zaidi ya miaka 40, alieleza matumaini kwamba kupitia mafunzo na vifaa walivyopokezwa, hali yao ya kiuchumi itaboreka.
“Nimekuwa na gharama ya Sh4,200 kuweka mafuta mashuani kila siku. Unaenda safari ndefu kutafuta samaki baharini na kisha mara nyingine unakosa kuvua chochote, hivyo kukadiria hasara tu,” akasema Bw Shee.