Gachagua abadili mikakati kuhusu kesi yake, aondoa dai la upendeleo dhidi ya majaji
ALIYEKUWA Naibu Rais Rigathi Gachagua ameondoa madai ya upendeleo dhidi ya jopo la majaji watatu wa Mahakama Kuu, hatua inayoashiria mabadiliko ya kimkakati huku akielekeza nguvu zake katika kesi kuu zinazopinga kuondolewa kwake mamlakani.
Katika mawasilisho mapya mbele ya Mahakama ya Juu, Bw Gachagua ameondoa rufaa yake ya ziada iliyolenga kubatilisha uamuzi wa Mahakama ya Rufaa ya Kenya ulioruhusu majaji hao kuendelea kusikiliza kesi hiyo.
Jopo hilo linaundwa na majaji Eric Ogolla, Anthony Mrima na Fredah Mugambi, ambao Bw Gachagua alikuwa amewashutumu kwa madai ya upendeleo na mgongano wa maslahi.
Kupitia wakili wake Kamotho Njomo, Bw Gachagua aliambia mahakama kuwa suala hilo limepitwa na wakati kufuatia uamuzi wa Mahakama ya Juu kukataa kusimamisha kesi inayoendelea katika Mahakama Kuu.
Kwa mujibu wa notisi ya Mei 4, 2026, upande wake ulisema kuwa rufaa hiyo haina tena maana kwa kuzingatia kanuni inayotumika pale ambapo suala linalobishaniwa halina athari ya moja kwa moja tena.
“Mahakama hii tukufu ilipokataa kutoa amri ya kusimamisha kesi katika Mahakama Kuu, rufaa hii ilipitwa na wakati. Kwa hivyo, mlalamishi wa kwanza anaondoa rufaa hii kikamilifu,” ilisema sehemu ya notisi hiyo.
Hatua hiyo inafuatia mvutano wa muda mrefu wa kisheria uliovuka ngazi tatu za mahakama tangu Bw Gachagua aondolewe madarakani Oktoba 2024, kupitia mchakato wa kisiasa uliotikisa ulingo wa siasa nchini.
Kwa mujibu wa wakili Njomo, uamuzi huo unalenga kuhakikisha juhudi zote sasa zinaelekezwa katika kesi kuu inayosikilizwa katika Mahakama Kuu ya Milimani, Nairobi.
Alisema kuwa suala la madai ya upendeleo tayari lilishughulikiwa na Mahakama ya Rufaa na halitapingwa tena.
“Tulikuwa tumewasilisha rufaa kupinga uamuzi huo, lakini sasa tumeamua kuiondoa ili kuangazia kesi kuu katika Mahakama Kuu,” alisema.
Awali, Bw Gachagua alikuwa ameomba majaji Ogolla, Mrima na Mugambi wajiondoe kwenye kesi hiyo akidai hawakuwa na uwezo wa kuisikiliza kwa haki.
Hata hivyo, katika uamuzi wake wa Mei 2025, Mahakama ya Rufaa ilitupilia mbali madai hayo, ikisema hayakuwa na msingi wa kutosha.
Mahakama hiyo ilieleza kuwa haikupata ushahidi wowote wa kuonyesha mgongano wa maslahi au mwenendo usiofaa kwa upande wa majaji hao.
“Hatuoni sababu yoyote ya kuwazuia majaji hao kusikiliza kesi hizi zilizounganishwa. Hatukuona upendeleo au ukosefu wa usawa katika mwenendo wao,” ilisema mahakama.
Mzozo huo unatokana na hatua ya Naibu Jaji Mkuu Philomena Mwilu kuunda jopo hilo Oktoba 2024, kusikiliza kesi mbalimbali zilizokuwa zinapinga kuondolewa kwa Bw Gachagua mamlakani.
Hata hivyo, Mahakama ya Rufaa ya Kenya iliamua Mei, 2025 kuwa hakuwa na mamlaka ya kufanya hivyo chini ya Kifungu cha 165(4) cha Katiba.
Baada ya uamuzi huo, Jaji Mkuu Martha Koome, aliunda upya jopo hilo kwa njia sahihi ya kisheria, hatua iliyorekebisha kasoro iliyokuwa imeibuliwa awali.
Licha ya kurekebishwa kwa utaratibu huo, Bunge la Kitaifa liliwasilisha rufaa katika Mahakama ya Juu likitaka kubatilisha uamuzi wa Mahakama ya Rufaa kuhusu mamlaka ya Naibu Jaji Mkuu.
Bw Gachagua naye aliwasilisha hoja akidai kuwa Bunge lilikuwa linachukua misimamo kinzani kuhusu suala hilo katika kesi tofauti.
Hata hivyo, kwa kuondoa rufaa yake, Bw Gachagua ameonyesha nia ya kupunguza kesi na kuepuka mvutano wa kisheria unaoweza kuchelewesha kusikizwa kwa kesi kuu.