Siasa

Sifuna afichua sifa za mgombea urais wanayemtaka katika kundi lao

Na MWANGI MUIRURI May 6th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

SENETA wa Nairobi Edwin Sifuna Jumanne aliwahakikishia wafuasi wa upinzani kuwa kutakuwa na mgombea mmoja wa urais atakayechaguliwa kupitia maoni ya wananchi ili kumkabili Rais William Ruto katika Uchaguzi Mkuu wa 2027, akisema kuwa ubinafsi hautavumiliwa.

Alisema kundi la Linda Mwananchi ndani ya chama cha ODM, limejitolea kuunda muungano mkubwa wa upinzani utakaotoa mgombea wa urais mwenye maadili mema, “mtu mwenye moyo mwema asiyezoea kufanya maovu.”

Kwa sasa mjadala ni nani kati ya Dkt Ruto, Kalonzo Musyoka, Rigathi Gachagua, Fred Matiang’i, Martha Karua, David Maraga, George Natembeya, Okiya Omtatah, Justin Muturi na wengine, anayekidhi vigezo hivyo.

“Kwa sasa, tuko katika mwelekeo sahihi. Jinsi serikali inavyopambana na upinzani kwa nguvu ni ishara kwamba tunaitikisa,” alisema alipokuwa akizungumza kwenye kipindi cha asubuhi cha Inooro FM.

Akijibu wito wa kutangaza azma yake ya urais, Bw Sifuna alisema hatakuwa kiongozi anayefuata matamanio yake binafsi na kugombea ili tu kufurahisha wafuasi, huku akigawanya upinzani.

Pia alisisitiza kuwa hayuko tayari kuwasaliti Wakenya kwa kukubali uteuzi katika serikali ya Rais Ruto.

“Urais si kuhusu mikutano mikubwa pekee. Tunataka mchakato jumuishi unaozingatia maslahi mapana ya taifa. Tunataka mgombea atakayekidhi angalau vigezo sita muhimu. Usaliti kwa Wakenya hautakubaliwa,” alisema.

Alitaja vigezo hivyo kuwa ni uadilifu, kuheshimu utawala wa sheria, kuzingatia uwezo katika uteuzi, kupambana na ufisadi, kuimarisha umoja wa kitaifa na kuheshimu taasisi, akidai kuwa Rais Ruto anakosa sifa hizo.

Bw Sifuna alionya kuwa upinzani uliogawanyika utakuwa pigo kwa Wakenya wengi wanaolalamika kuwa hawawezi kuvumilia muhula mwingine wa utawala wa sasa.

“Ni lazima tuungane na kusimamisha mgombea mmoja dhidi ya Rais Ruto,” alisisitiza.

Aliongeza kuwa kazi iliyo mbele yao si rahisi, akimtaja Rais Ruto kama mwanasiasa mwenye uzoefu mkubwa.

“Tunachohitaji ni umoja. Hatuhitaji wagombea wengi. Tunahitaji mazungumzo ya kweli na ya wazi ili kumkabili kama nguvu moja.”

Bw Sifuna alisema hataki kuona Rais Ruto akirejea madarakani kwa ushindi mwembamba kama wa kura 200,000 uliompa ushindi mwaka 2022.

“Hatuwezi kumudu ubinafsi,” alisema.

Alisema kundi lao linafuata maono ya Raila Odinga, akimtaja kama kiongozi mwenye moyo wa kusamehe.

Alitoa mfano wa jinsi Odinga alivyomsamehe Rais wa zamani Daniel arap Moi licha ya kufungwa jela kwa miaka tisa na kunyimwa nafasi ya kumzika mama yake.

“Odinga alitufundisha kuwa kisasi hakiwezi kujenga taifa. Alitukumbusha pia jinsi Nelson Mandela alivyowasamehe waliomtesa wakati wa ubaguzi wa rangi. Hayo ndiyo maadili tunayoyafuata,” alisema.

Bw Sifuna alibainisha kuwa Wakenya wanastahili serikali yenye viongozi watulivu na wanaojali matarajio ya wananchi ya ukombozi wa kweli.

Alidai kuwa ishara kuwa serikali ina hofu ni jinsi inavyomshambulia Rais mstaafu Uhuru Kenyatta, ikimlaumu kwa kufadhili upinzani.

“Serikali iliyo na idara zote za usalama haipaswi kutegemea propaganda,” alisema.

Kwa mujibu wake, serikali ina hofu na ushawishi wa Bw Kenyatta katika eneo la Mlima Kenya, akisema kura za eneo hilo ni muhimu sana katika uchaguzi ujao.

Aliwataka wakazi wa Mlima Kenya kufuata mwongozo wa Bw Kenyatta ifikapo 2027 na kuungana na Wakenya wengine kuleta mabadiliko.

Aidha, alikosoa vikali hoja ya Seneta wa Nandi Samson Cherargei ya kuondoa marupurupu ya Rais mstaafu, akisema ni siasa za kujitafutia umaarufu.

“Marupurupu hayo yanalindwa na Katiba. Hayawezi kuondolewa kwa hoja ya Seneti,” alisema, akiongeza kuwa serikali inaonyesha hofu kupitia hatua kama hizo huku upinzani ukiendelea kushinikiza mabadiliko.