Amerika, Iran waweka wazi makubaliano yao ya kusitisha vita
WASHINGTON, Amerika:
AMERIKA na Iran Alhamisi, Juni 18, 2026 zilianika yaliyomo kwenye makubaliano yao ya muda ambayo yametiwa saini na marais wao ili kumaliza vita ambavyo vimedumu tangu Februari.
Rais Donald Trump ametishia kuwa iwapo mkataba huo hautaheshimiwa na Iran, atarejelea vita na kuangamiza maafisa wa serikali ya Iran.
“Tutawalipua kwa mabomu iwapo watakosa kuheshimu mkataba huu. Ili nisifanye hivyo, lazima waheshimu mkataba huu,” akasema Trump.
“Iwapo watakosa kuniridhisha na wakiuke mkataba huu, tutarudi na kuwaangushia mabomu kichwani,” akaongeza.
Makubaliano hayo yana hoja 14 na yamesitisha vita kwa siku 60 ikiwemo mashambulizi ya Israel dhidi ya Lebanon.
Trump alitia saini nakala iliyoandikwa kwa Kingereza huku Rais wa Iran Masoud Pezeshkian, akitia saini ile iliyoandikwa kwa lugha ya Kiarabu.
Baada ya makubaliano hayo, maafisa wa Amerika na Iran bado wanaendelea na mazungumzo ambayo yanatarajiwa kukamilika baada ya siku 60.
Trump anaamini baada ya siku 60, amani itarejea kabisa katika Ukanda wa Mashariki ya Kati.
Viongozi wa Iran hawakumjibu Trump kuhusu vitisho vyake vipya huku wakisherehekea na kusema makubaliano hayo yamejaa matakwa yao.
Huu ulikuwa mkataba wa kwanza kutiwa saini na marais wa Iran na Amerika tangu Iran ijitangaze Jamhuri ya Kiislamu baada ya mageuzi ya kisiasa ya 1979.
“Kupitia uwezo wa jeshi letu, tumeafikia malengo yetu kwa njia ya mazungumzo,” akasema Mohammad Baqer Qalibaf aliyeongoza mazungumzo kwa upande wa Iran.
Amerika na Israel zilivamia Iran mnamo Februari 28 na kumuua Kiongozi wa kidini nchini humo Ayatollah Khamenei na viongozi wa ngazi ya juu wa jeshi la nchi hiyo.
Vita hivyo, vilienea kwenye ukanda wa Mashariki ya Kati na vimechangia maafa ya zaidi ya watu 7,000 wengi wao kutoka Iran na Lebanon.
Pia vimetatiza usambazaji wa mafuta ulimwenguni na kupandisha bei yake pamoja na bei ya chakula.