Habari za Kitaifa

Haitatusaidia kulaumiana, asema Ruto akizindua fidia ya Sh2bn kwa wahanga wa maandamano

Na DANIEL OGETTA June 16th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WAHASIRIWA zaidi ya 1,000 wa ukiukaji wa haki za kibinadamu, ikiwemo ukatili wa polisi na vyombo vya dola kutumia nguvu kupita kiasi, wataanza kupokea malipo yao fidia kuanzia wiki ijayo.

Hii ni baada ya serikali kuidhinisha mpango wa fidia na kutenga Sh2 bilioni kwa shughuli hiyo.

Haya yamejiri kufuatia ufanisi wa kuwatambulisha na kuidhinisha wahasiriwa, katika kile Rais William Ruto alitaja kuwa mwanzo wa mwisho wa ukurasa wenye uchungu katika historia nchini.

Wahasiriwa watakaofidiwa wanatoka vitengo sita vya dhuluma ikiwemo haki ya kuishi (wahasiriwa 245), dhuluma za ngono (75), uhuru kutokana na mateso (135), uhuru na usalama wa mtu binafsi (473), haki ya mali (138) na kutoroshwa kimabavu (35).

Dkt Ruto jana alisema ni hatua ya kujitolea iliyotokana na msimamo kuwa Kenya haiwezi kuendelea kusafiri ikitumia barabara ile ile yenye uchungu, kizazi baada ya kizazi, maandamano baada ya maandamano, mkasa baada ya mkasa.

Alikuwa akizungumza kwenye hafla ya kuzindua mpango wa malipo na fidia kwa wahasiriwa wa dhuluma za haki za kibinadamu wakati wa maandamano.

Dhuluma zilizorekodiwa ni kutoka 2017-2022 zilizohusishwa pakubwa na malalamishi kuhusu uchaguzi mkuu; ukiukaji wa haki katika maandamano ya 2023 na 2024 hasa yale ya Gen Z ya kupinga Mswada wa Fedha; na 2025 wakati wa maandamano ya Saba Saba.

Mchakato wa uthibitishaji ulielekezwa na “msingi razini wa kuamini”, kiwango cha ushahidi, kuambataba na taaluma ya haki za kibinadamu kimataifa, ilisema KNCHR.

“Kwa muda mrefu, kila mara Wakenya wametumia haki hizi, aghalabu matokeo yamekuwa dhuluma za kikatili, majeraha, kupoteza maisha, uharibifu wa mali, machungu na migawanyiko. Familia zimewazika wapendwa.

“Vijana wamebeba makovu kimwili na kihisia. Biashara zimeharibiwa. Maafisa wa polisi wamejeruhiwa. Jamii zimeachwa na matatizo kisaikolojia,” alisema Rais Ruto.

Akikiri kwamba kumekuwepo visa ambapo hatua iliyochukuliwa dhidi ya maandamano ya umma imesababisha matumizi ya nguvu kupita kiasi, ukiukaji wa haki na kupoteza maisha, Rais alisema kila mara mkondo huo unapozuka “Kenya hupoteza (na) demokrasia yetu hudidimia. Kisha lawama huanza.”

Machi mwaka huu Dkt Ruto aliagiza KNHCR kubuni na kuwasilisha mwongozo wa malipo ya fidia kwa wahasiriwa wa dhuluma za haki za kibinadamu katika muda wa siku 60.