Habari za Kitaifa

Serikali ya Ruto yaendeleza ukaidi wa maagizo ya korti licha ya kiapo cha kufuata sheria

Na JOSEPH WANGUI June 16th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

RAIS William Ruto aliingia madarakani mnamo 2022 kwa ahadi ya kuongoza serikali inayozingatia utawala wa sheria.

Aliwahakikishia Wakenya mara kwa mara kwamba amri za mahakama zingeheshimiwa bila kujali zinaathiri huduma za serikali au la.

Lakini miaka minne baada ya hapo, majaji sasa wanashinikizwa kuwalazimisha maafisa wa serikali kutii sheria, ilhali wao ndio walikabidhiwa jukumu la kulinda Katiba.

Mawaziri, makatibu wakuu, wakuu wa polisi na viongozi wa taasisi za kikatiba ni kati ya wanaoandamwa na kesi za kudharau mahakama.

Mgogoro wa hivi punde ni kati ya Waziri wa Afya Aden Duale na maafisa wa Wizara ya Afya wanaotuhumiwa kupuuza amri za mahakama zilizositisha kujengwa kwa kituo cha kuwatenga wagonjwa wa Ebola.

Kituo hicho kinastahili kujengwa katika kambi ya jeshi ya Nanyuki Kaunti ya Laikipia kwa ajili ya raia wa Amerika ambao wamepatwa na ebola ndani na nchi.

Katiba Institute na Chama cha Wanasheria Nchini (LSK) zinasema mradi huo unaoungwa mkono na Amerika unaendelea licha ya mahakama kuingilia kati.

“Wamepuuza amri hizi kwa sababu kuna ripoti nyingi zinazoonyesha kuwa wanaendelea na ujenzi wa kituo hicho,” akasema wakili wa Katiba Institute, Malidzo Nyawa. Hata hivyo, Bw Duale alikanusha madai hayo na kusema serikali ya Rais Ruto inafuata sheria.

“Sisi ni serikali inayoheshimu sheria na tunatii amri za mahakama,” akasema Bw Duale.

Kesi hii ni miongoni mwa nyingine kadhaa ambapo serikali imekaidi mahakama.

Katika Kaunti ya Meru, Katibukatika Idara ya Misitu Gitonga Mugambi amekuwa akisisitiza ujenzi wa ikulu na uwanja wa ndege ndani ya Msitu wa Imenti utaendelea licha ya amri wa mahakama.

Mitambo ya ujenzi iliingizwa msituni chini ya ulinzi mkali huku wakazi na wanaharakati wa mazingira wakipinga hatua hiyo.

Katibu wa Ulinzi, Patrick Mariru naye anakabiliwa na madai ya kudharau mahakama baada ya serikali kushindwa kulipa zaidi ya Sh200 milioni zilizotolewa na mahakama kwa wanajeshi wa zamani walioteswa kufuatia jaribio la mapinduzi la 1982.

Mahakama ilikataa hoja ya ukosefu wa fedha kama sababu ya kuchelewesha malipo hayo kwa miaka mingi. Kesi hiyo bado inaendelea Mahakama ya Milimani, Nairobi.

Inspekta Jenerali wa Polisi Douglas Kanja pia amekabiliwa kwa kudharau mahakama, baada ya polisi kushindwa kutii amri ya mahakama na kumrejeshea aliyekuwa Waziri wa Utumishi wa Umma Justin Muturi walinzi wake.

Spika wa Bunge la Kitaifa Moses Wetang’ula naye alipuuza uamuzi wa Mahakama Kuu mnamo Februari 2025 uliobaini kuwa mrengo wa Azimio ndio ulikuwa na idadi ya wabunge wengi kuliko ule wa Kenya Kwanza.