Hospitali za rufaa zaugua kwa uhaba wa madaktari, fedha na vifaa
HOSPITALI tatu kubwa za rufaa nchini zinakabiliwa na upungufu wa wahudumu muhimu na misongamano, kipindi hiki ambapo wataalamu wenye tajriba wanaondoka kuchuma riziki Uropa, Amerika na Mashariki ya Kati.
Hospitali hizo tatu; Hospitali ya Mafunzo na Rufaa ya Moi, (MTRH), Hospitali Kuu ya Kenyatta (KNH) na Hospitali ya Mafunzo na Rufaa Kaunti ya Nakuru, zinahangaika kutoa huduma bora za matibabu, Taifa Leo imefichua.
Hospitali ya Rufaa ya Moi jijini Eldoret, kwa mfano, inakabiliwa na uhaba wa wafanyakazi wa afya, ikipungukiwa na takriban wauguzi 1,000.
Kulingana na ripoti mpya ya Mkaguzi wa Hesabu za Serikali, Nancy Gathungu, kwenye bajeti iliyokamilika Juni 2025, hospitali hiyo ina uhaba wa wahudumu wa afya wasiopungua 1,032 ikiwemo wauguzi.
Rekodi za wafanyakazi zinaashiria hospitali hiyo, kwa mfano, ina wapasuaji wakuu watano badala ya 11, matabibu sita wa saratani badala ya 14, maafisa wa matibabu 73 badala ya 83, madaktari 15 wa watoto badala ya 18 inayohitajika na wataalam tisa wa mashine za matibabu badala ya 14.
Hospitali hiyo inayostahili kuwa na wauguzi 1,000 ina chini ya 1,000.
“Upungufu huo umeathiri pakubwa utoaji huduma za afya katika hospitali ya pili kubwa zaidi ya rufaa nchini,” anaeleza Bi Gathungu kwenye ripoti.
Taifa Leo ilibaini kuwa changamoto hiyo inasababishwa na “kuhama” ambapo wauguzi na madaktari wenye tajriba kati ya 60-100 hujiuzulu kila mwaka kuajiriwa Uropa, Amerika na Mashariki ya Kati.
Hospitali ya Mafunzo na Rufaa Nakuru, kituo kikubwa zaidi Bonde la Ufa Kusini, inayohudumia Nakuru na kaunti nyingine zaidi ya sita ikiwemo Baringo, Kericho, Narok, Nyandarua, Laikipia, na Narok, vile inang’ang’ana na uhaba wa wahudumu na msongamano.
Ziara ya Kamati ya Afya Jumanne ilifichua kwamba madaktari wawili wanalazimika kuhudumia wagonjwa wasiopungua 1,000 kwa siku.
KNH, vilevile inakabiliwa na uhaba wa wahudumu wa afya na msongamano ambapo ripoti mpya ya Mkaguzi Mkuu inafichua kuwa kituo hicho kinakabiliwa na changamoto la vitanda.
“Tathmini ya takwimu za wagonjwa waliolazwa ilifichua kuwa hospitali hiyo ilirekodi kiwango cha jumla cha vitanda asilimia 26 na wadi kadhaa za dawa, upasuaji wa jumla, watoto na matibabu maalumu ziliandikisha zaidi ya asilimia 140,” inasema ripoti.
Mgao wa chini kwenye bajeti umeathiri hosputali hiyo ambapo ilirekodi upungufu wa Sh4.9 bilioni kwenye bajeti ya Sh22.5 bilioni ya 2024/2025.
Malalamishi ya muda mrefu ikiwemo uhaba wa wahudumu na mazingira duni ya kazi ni sehemu ya masuala ualiyosababisha mgomo uliofutiliwa mbali Jumanne baada ya pande husika kuafikiana kuhusu mkataba wa kurejea kazini.